Rais wa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo ,Joseph Kabila ni sharti aheshimu katiba na kujiuzulu mwishoni mwa muhula wake ,waziri wa maswala ya kigeni nchini Ufaransa Jean-Mark Ayrault amesema katika mahojiano na kituo cha habari cha TV5.

Bwana Ayrault alikuwa akisisitiza wito aliotoa wiki iliopita wakati akiwahutubia wanafunzi mjini Paris.
Wakati huu aliangazia madai kwamba Ufaransa imekuwa ikiingilia maswala ya ndani ya DRC,akisema kuwa taifa lake haliko pekee kumkumbusha Kabila kwamba lazima aheshimu sheria.
Aliambia kituo hicho: ''Rais Kabila lazima aonyeshe mfano mwema. Ni lazima aheshimu katiba. Iwapo vikwazo vitahitajika tutaamua kuvitekeleza. Nataka watu waelewe; Watu waliopo katika mamlaka DRC ni lazima wawajibike. Iwapo wanahitaji amani nchini mwao, iwapo wanajali hali ya watu wao ,ni lazima wafuate katiba''.
Lakini serikali ya DRC imesema Ufaransa inachochea maasi dhidi ya serikali nchini humo.
Waziri wa mawasiliano Lambert Mende ameambia shirika la habari la AFP kwamba Ufaransa 'inacheza mchezo hatari'.
"Baada ya kuwasha moto na kuwahimiza watu wenye misimamo mikali, Ufaransa itawaondoa raia wake na kuwaacha raia wa Congo taabani," ameambia wanahabari.
"Wasiwasi wa Waziri Ayrault kuhusu DRC unazua shaka kwa sababu unafufua kumbukumbu za uingiliaji kati ambao ulizaa vurugu Libya.