Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndali
BAADA ya uamuzi wa kuwafukuza vyuo walimu wanne waliokuwa kwenye mafunzo ya vitendo katika Shule ya Sekondari ya Kutwa ya Mbeya (Mbeya Day), serikali imesema vyuo husika vinaweza kushauri adhabu mbadala iwapo vitajiridhisha kuwepo kwa mazingira tofauti na yaliyozingatiwa kwenye uamuzi wa kuwafukuza vyuo.
Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako alisema hayo juzi alipozungumza na waandishi wa habari mkoani Mbeya alikokuwa katika ziara kwenye shule mbalimbali mkoani humo.

Profesa Ndalichako alisema uamuzi uliochukuliwa na ofisi yake ulizingatia sheria ndogo zilizotungwa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udsm) zinazoainisha makosa yanayoweza kumfukuzisha chuo mwanafunzi.
Hata hivyo, alisema uamuzi uliochukuliwa unaweza kutazamwa upya na vyuo husika iwapo uzito uliochukuliwa na wizara utaonekana kuwa katika mazingira na uhalisia wa tukio husika.
Walimu wanne waliokuwa kwa vitendo katika shule ya Mbeya Day walifukuzwa vyuo baada ya uamuzi wa serikali kutokana na kuhusika kumpiga mwanafunzi Sebastain Chinguku vibao, mateke na fimbo kwa ukatili Septemba 28 mwaka huu shuleni humo.
Walimu hao walibainika baada ya kipande cha video kusambazwa katika mitandao ya kijamii hivi karibuni. Waliohusika na vyuo walivyokuwa wakisoma ni Frank Msigwa (anayedaiwa kumpiga zaidi mwanafunzi makofi kichwani), John Deo na Sante Gwamaka wote wa DUCE-UDSM, na Evans Sanga wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.
Akijibu swali la idadi ipi ya viboko inastahili kutolewa kama adhabu kwa mwanafunzi anayekwenda kinyume na maelekezo ya shule yake, Profesa Ndalichako alisema binafsi asingependa mwanafunzi achapwe hata kiboko kimoja lakini hilo linawezekana pale wanafunzi watakapozingatia maadili.
“Adhabu yoyote kwa mwanafunzi inatolewa pale anapokuwa amekwenda kinyume na maadili ya shule yake. Kama wanafunzi wote watazingatia maadili sidhani kama kuna mwalimu atakayempiga mwanafunzi hata kiboko kimoja. Haya yote yanatokea kutokana na wanafunzi kukosa nidhamu,” alisisitiza Ndalichako.
Aliwasihi wanafunzi kuzingatia maadili ya shule yao, akisema ndiyo njia pekee ya kuwawezesha kuishi vyema na walimu wao na pia kufanya vyema kitaaluma na kuwasihi wazazi kuwafundisha watoto wao nidhamu ya kuwaheshimu watu wote, akisema malezi hayo yatawapunguzia walimu adha ya kuishi na wanafunzi watukutu ambao kimsingi wanazorotesha utendaji kazi wao.
Katika hatua nyingine, wizara hiyo imesema Waraka wa Elimu wa mwaka 2002 namba 24 unaelekeza utoaji wa adhabu ya viboko kwa wanafunzi kuwa ni lazima kuidhinishwa na mwalimu mkuu kwa maandishi huku kukiwa na daftari linaloonesha idadi ya viboko alivyopigwa mwanafunzi na mwalimu aliyemchapa.
Wizara hiyo imeweka bayana utoaji wa adhabu hiyo, lakini imewataka wanafunzi kujiepusha kufanya makosa mbalimbali yatakayosababisha kupigwa viboko kwani shuleni wameenda kwa ajili ya kusoma.
Kaimu Kamishna wa Elimu, Nicholaus Buretta alisema hayo juzi alipozungumza na gazeti hili kuhusu adhabu anayopaswa kupewa mwanafunzi na suala zima la maadili kwa wanafunzi na walimu.
Alisema adhabu hiyo ya viboko hutolewa kwa kuangalia ukubwa wa kosa, jinsi ya mwanafunzi, afya yake pamoja na kuhakikisha viboko hivyo havizidi vinne kwa mwanafunzi tena hutolewa na mwalimu mkuu au mwalimu aliyethibitishwa na mwalimu mkuu kwa maandishi.
“Katika adhabu hiyo ni lazima mtoto wa kike apigwe viboko na mwalimu wa kike labda kama shule hiyo haina mwalimu wa jinsia hiyo, hivyo mwalimu mkuu atatoa maelekezo ya jinsi ya kumuadhibu. “Hatuhamasishi adhabu hii kwa wanafunzi, bali wanafunzi wanatakiwa kujua kuwa wamekuja shuleni kusoma na hawajaja kuchapwa viboko, hivyo lazima wajiepushe kufanya makosa yatakayosababisha kuchapwa, huku tukihamasisha mahusiano bora kati ya mwalimu na mwanafunzi ambayo ni yale ya kama mzazi,” alisema Buretta.
Buretta alisema katika kuboresha uhusiano baina ya walimu na wanafunzi, wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) itahakikisha wanafikia wastani wa darasa moja kuwa na wanafunzi 1:40 hadi 45.
Kwa upande wao, Shirikisho la Wamiliki na Mameneja wa Shule na Vyuo binafsi Tanzania (Tamongsco) limetaka walimu kufuata waraka maalumu wa serikali katika kuadhibu wanafunzi, ikiwa ni pamoja na kuwa karibu na wanafunzi mara wanapokosea.
Imeandikwa na Joachim Nyambo, Mbeya na Theopista Nsanzugwanko, Dar es Salaam.