Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma amewataja watu wanaofanya maandamano dhidi yake kuwa wabaguzi wa rangi akisema walibeba mabango yalioonyesha kuwadharau watu weusi.
Maelfu ya waandamanaji walifanya maandamano baada ya kumfuta kazi waziri wake wa fedha Pravin Gordan.

Maandamano hayo yalipangwa na vyama kadhaa vya upinzani na makundi kadhaa ya wanaharakati.
''Maandamno yaliofanyika wiki iliopita yalibaini kwamba ubaguzi wa rangi upo na unaendelea nchini Afrika Kusini'', alisema.
Wakati huohuo wafuasi wa rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma walivuruga hafla ya makumbusho ya aliyekuwa mwanaharakati wa kupambana na ubaguzi wa rangi, Ahmed Kathrada.
Watu hao walianza kuleta uzushi wakati aliyekuwa waziri wa fedha Pravin Gordan alipokuwa anatoa hotuba yake ambayo ilikuwa inakashifu ufisadi katika chama cha ANC, akisema kuwa huenda chama hicho hakitashinda uchaguzi wa 2019.
Waandamanaji wanaopinga uongozi wa rais Zuma
Image captionWaandamanaji wanaopinga uongozi wa rais Zuma
Umati ulianza kuimba nyimbo za kumsifu Zuma ambaye amekumbwa na kashfa baada ya nyingine.
Hafla hiyo ya Kathrada ilikuwa ikiendelea KwaZulu-Natal ambapo umati huo ulimsifu rais Zuma kwa kumpiga kalamu Gordan.
Akijaribu kuipaza sauti yake juu ya kelele wa umati, Gordan alisema, " ikiwa tutaendelea kuzozana tutapoteza imani ya watu wa Afrika Kusini kwetu.
Tunataka kubaki serilkalini ili tuibadilishe Afrika Kusini."
Wiki ijayo, Zuma anatarajiwa kupambana na kura ya kutokuwa na imani dhidi yake ambayo inafadhiliwa na upinzani.
Anadaiwa kuwa kiongozi fisadi ambaye anataka kuwajaza rafiki zake kwenye wizara ya fedha.
Rafiki zake Zuma hata hivyo wanakanusha madai hayo huku wakisema kuwa Zuma ana nia tu ya kuendeleza mabadiliko makubwa ya kiuchumi itakayonufaisha nchi.
Mahakama ilitoa amri mwaka jana ikisema kuwa Zuma alivunja kiapo chake cha kazi kwa kukosa kulipa serikali pesa zilizotumiwa kuboresha makazi yake ya kibinafsi na kutaka ashtakiwe kwa kosa la ufisadi.
Zuma anasema yeye hana makosa yoyote.