Mwanamziki maarufu wa rhumba Koffi Olomide amenyimwa kuingia nchini Zambia kutokana na makosa mengi yanayomkabili katika taifa hilo la kusini mwa Afrika na Ufaransa ikiwemo madai ya kumshambulia mpiga picha katika hafla moja ya mziki alipokuwa ziarani nchini humo.

Pia, anakabiliwa na madai ya kuwanyanyasa kingono wachezaji wake wa densi, kuwateka nyara pamoja na kuwaajiri kwa njia ya udanganyifu kutumia vibali ghushi.
Kabla ya ziara hiyo yake iliyopigwa marufuku kwa sasa, Olomide - anayeishi Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo, ameitaja Zambia kuwa "makazi yake ya pili" na kuongeza kuwa angependa kupiga shoo nchini humo "kabla afe."
Taarifa ya kuomba msamaha kutoka msanii huyo wa miaka 62 imepeperushwa kwenye kituo kimoja cha radio nchini Zambia. Amefunguka kuwa anawapenda wanawake wa Zambia huku akikwepa madai dhidi yake bila kuyaangazia.
Olomide, majina kamili Antoine Christophe Agbepa Mumba, alitarajiwa kuandaa burudani katika maonyesho mawili nchini Zambia mwezi huu, lakini serikali imetishia kuwa itamtia pingu pindi atakapotua taifa hilo.
Ubalozi wa Ufaransa nchini Zambia imejiunga na juhudi za kumkamata msanii huyo huku ikiitisha kukamatwa kwake siku ya Jumamosi wiki hii.
Balozi wa Ufaransa nchini humo, Sylvain Berger, ametishia kuwashirikisha maafisa wa usalama wa Interpol kumkamata Olomide, aliyesema kuwa bado mashataka dhidi yake nchini Ufaransa hayajafutiliwa mbali.
Nyota huyo wa rhumba - aliyejizolea sifa kwa mtindo wake wa mavazi na maisha ya anasa na kifahari - sio mgeni kwa sakata na utata.
Koffi Olomide atoa wimbo mpya kuwaomba msamaha akina mama Afrika
Mnamo 2016, alinaswa kwenye Kamera akimlisha teke mmoja wapiga densi wake alipowasili nchini Kenya. Alitolewa taifa hilo kwa haraka.
Mwaka wa 2012, alipatikana na hatia ya kumshambulia msimamizi wake Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Alihukumiwa kwa kifungo kilichoahirishwa cha miaka mitatu.
Mabishano yake na msimamizi huyo, Diego Lubaki, ilikuwa ni juu ya madeni dola $3,700 , mahakama ilifahamu.
Mnamo mwaka wa 2008, alidaiwa kumpiga mpiga picha wa Shirika la habari la kibinafsi la RTGA na kuvunja kamera yake baada ya kumvamia katika sehemu moja ya burudani mji mkuu wa Kinshasa, baada ya kutofautiana kuhusu vibali vya kupiga picha.
Mwishowe, spika wa bunge la kitaifa aliingilia kati na kusuluhisha mtafaruku huo huku akituliza uhasama kati ya mwimbaji huyo na mmiliki wa runinga hiyo.