Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba akisalimiana na Waziri
wa biashara na ushirika nchini Uganda Mhe Fredric Ngobi Gume muda mchache
kabla ya kuanza kwa mkutano wa mawaziri wa nchi hizo mbili, mkutano
uliohudhuriwa pia Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage,
Jana 11 Julai 2018. (Picha zote Na Mathias Canal, WK)

Kikao kikiendelea eneo la Mtukula Wilayani Misenyi. Jana 11 Julai 2018
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage akisalimiana
na Waziri wa biashara na ushirika nchini Uganda Mhe Fredric Ngobi Gume muda
mchache kabla ya kuanza kwa mkutano wa mawaziri wa nchi hizo mbili, mkutano
uliohudhuriwa pia na Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba, Jana 11
julai 2018.

Mathias Canal-WK, Mtukula-Kagera

Serikali
ya Uganda imeeleza kuvutiwa na uendeshaji wa ushirika nchini Tanzania hivyo
imeomba kupata ridhaa ya kuzuru nchini Tanzania ili kujifunza namna bora ya
uendeshaji wa ushirika.

Ombi
hilo limetolewa jana 11 Julai 2018 na Waziri wa Biashara na Ushirika nchini
Uganda Mhe Fredrick Ngobi Gume wakati akizungumza kwenye mkutano uliohudhuriwa
pia na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage uliofanyika
katika eneo la Mtukula Wilayani Misenyi.

Katika
mkutano huo Waziri huyo  anayeshughulikia Ushirika nchini Uganda
alimpongeza Waziri wa Kilimo nchini Mhe Dkt Charles Tizeba kwa Nazi kubwa
aliyoifanya katika kipindi cha muda mfupi kurejesha imani kubwa na ushirika kwa
wakulima ambapo alimpongeza pia kwa tuzo ya heshima aliyokabidhiwa na Waziri
Mkuu wa Tanzania Mhe Kassim M. Majaliwa kwa niaba ya wana ushirika wakati wa
sherehe za kilele cha siku ya ushirika Duniani kwenye viwanja vya Furahisha
Jijini Mwanza.

Waziri
wa biashara na ushirika nchini Uganda Mhe Gume alimuhakikishia mwenyeji wake
kuwa biashara ya Kahawa nchini humo ina changamoto sawa katika nchi zote mbili
kwa kuwa swala la mikopo isiyo rasmi inayowanyonya wakulima (Butura) nchini
Uganda ipo kwa kiwango cha juu.

Alisema
kuwa serikali ya Uganda inayoongozwa na Rais wa nchi hiyo Mhe Yoweri Kaguta
Museveni itaendeleza ushirikiano na serikali ya Tanzania inayoongozwa na Mhe
Rais Dkt John Pombe Magufuli hivyo panapohitajika ushirikishwaji katika
biashara hususani kwenye sekta ya Kilimo watakuwa na msimamo wa pamoja.

Alisema
miongoni kwa mambo mengine ya kujifunza nchini Tanzania itakuwa ni pamoja na
kujifunza kuhusu namna bora  ya kuendesha ushirika na kuanzisha mfumo wa
stakabadhi ghalani.

Kwa
upande wake, Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba alimueleza Waziri Gume
kuwa njia mojawapo ya kusimamia ushirika ni pamoja na mkakati wa usimamizi
madhubuti ikiwa ni pamoja na kuwaweka kizuizini wabadhilifu wote katika
ushirika.

Mkutano
huo ni muendelezo wa utekelezaji wa maagizo ya Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli aliyoyatoa wakati akiwaapisha viongozi
mbalimbali Ikulu Jijini Dar es salaam tarehe 2 Julai 2018 na kuitaka Wizara ya
Kilimo kufuatilia kwanini wakulima wa zao la Kahawa wanacheleweshewa malipo yao
sambamba na kujua kwanini wakulima wanauza Kahawa yao nchini Uganda.

Naye
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage aliongeza kuwa
wakulima wa Tanzania na Uganda wanapaswa kuweka msisitizo katika Kilimo kwani
kufanya hivyo kutaongeza uimara na uanzishwaji wa viwanda vitakavyoongeza
chachu ya ajira kwa wananchi.

MWISHO