Matumaini ya Tanzania kufuzu katika fainali za kombe la mataifa ya Afrika (Afcon) 2019 yataamuliwa kesho watakaporudiana na Cape Verdea baada ya kukubali kipigo cha goli 3-0 juma lililopita.

Wakati Tanzania hali ikionekana kuwa ngumu kwa sasa, nchi jirani za Kenya, Uganda na Burundi hali zao zipo vizuri na kuna matumaini makubwa kuwa wanaweza kufuzu na kuuwakilisha ukanda wa Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) katika michuano hiyo itakayofanyika nchini Cameroon.
Tanzania imecheza michezo mitatu katika Kundi L na kuambulia pointi 2 baada ya kutoka sare mara mbili na kufungwa mchezo mmoja.
Kocha wa timu ya Tanzania maarufu kama Taifa Stars, Emmanuel Amunike bado hajakata tamaa, na anawataka Watanzania kuendelea kuwa na imani kuwa timu yao ina nafasi ya kuelekea Cameroon.
Amunike, ambaye ni nyota wa zamani wa Nigeria ameliambia gazeti la The Citizen la Tanzania kuwa; "nafasi bado ipo, kundi letu bado lipo wazi, tunaweza kufanikiwa."
Muelekeo wa safari ya Tanzania utajulikana kesho Jumanne watakaporudiana na Cape Verde, ni lazima washinde ili matumaini yao yawe hai. Kama hiyo haitoshi, itawapasa washinde walau mchezo mmoja na kutoka sare mwengine watakapochuana na Uganda na Lesotho.
Uganda maarufu kama Cranes wanaongoza Kundi L wakiwa na pointi 7 baada ya kushinda michezo miwili na kutoka sare mchezo mmoja. Cranes watahitaji alama 4 tu katika michezo mitatu iliyosalia ili wajihakikishie kufuzu.
Kwa upande wa Kenya, wanaongoza kundi F wakiwa na pointi 7 baada ya kucheza michezo minne na kushinda miwili, kupoteza mmoja na kutoka sare mmoja.
Mashabiki wa Uganda wakishangiliaHaki miliki ya pichaAFP/GETTY
Image captionUganda wapo katika nafasi nzuri ya kufuzu kwa kuongoza Kundi L kwa alama saba
Katika michezo miwili iliyosalia ambapo watacheza na Ghana jijini Accra, na Sierra Leone, Nairobi Harambee Stars wanahitaji kushinda mchezo mmoja na sare moja ili kufuzu.
Ethiopia ambayo pia inatoka ukanda wa Cecafa inashika nafasi ya pili katika kundi hilo wakiwa na alama 4 itakuwa na kibarua kizito kugombea nafasi ya kufuzu na Ghana wenye alama 3 na Sierra Leone wenye alama 2. Yeyote kati ya timu hizo tatu anaweza kuungana na kinara Kenya kufuzu.
Burundi nao wapo katika nafasi nzuri ya kufuzu kupitia Kundi C. Mpaka sasa Amavubi wana alama 5 baada ya kutoka sare michezo miwili na kushinda mmoja. Hatahivyo itawapasa wapigane vilivyo na Mali wenye pointi 7 na Gabon yenye alama 4 ili kumaliza katika nafasi mbili za juu na kufuzu.
Kutoka ukanda wa Cecafa tayari mataifa mawili yapo katika hali mbaya na uwezekano wa kufuzu ni mdogo. Sudani Kusini na Rwanda hawajaambulia hata alama moja kwenye mechi tatu walizocheza mpaka sasa.
Ili wafuzu, wote, itawapasa washinde mechi tatu walizosalia nazo, hali ambayo ni ngumu kuyumkinika. Hatahivyo mpira wa miguu ni mchezo mgumu kutabiri matokeo yake.