Data ya ndege ya Ethiopia iliokumbwa na ajali wiki moja iliopita inaonyesha kuwa ajali hiyo inafanana na nyengine iliotokea nchini Indonesia mwezi Oktoba , kulingana na waziri wa uchukuzi nchini Ethiopia.
Ndege zote mbili zilikuwa aina ya Boeing 737 Max 8. Jumapili iliopita ndege hiyo ya Ethiopia ilianguka baada ya kupaa kutoka mjini Addis Ababa na kuwaua takriban watu 157 walioabiri.

Waziri wa uchukuzi Dagmawit Moges aliambia waandishi wa habari kwamba ripoti ya uchunguzi itatolewa ndani ya siku 30.
Kufanana kama huko kulionekana kati ya ndege ya Ethiopia aina ya 302 na ile ya Indonesia Lion Flight 610 ambayo itatumika katika uchunguzi mwengine wakati wa uchunguzi huo, bi Dagmawit aliambia waandishi siku ya jumapili.
Katika visa vyote viwili data ilionyesha kwamba mwinuko wa ndege hiyo uliathirika baada ya ndege hiyo kupanda na kushuka kwa ghafla
Mazishi ya waathiriwa wa ajali ya ndege ya EthiopiaHaki miliki ya pichaAFP
Image captionMazishi ya waathiriwa wa ajali ya ndege ya Ethiopia
Mwenyekiti wa kampuni ya Boeing na afisa mkuu mtendaji Dennis Muilenburg baadaye alithibitisha kwamba kampuni hiyo inaunga mkono uchunguzi huo.
Katika taarifa, aliongezea kwamba Boeing ilikuwa inaendelea kuimarisha programu yake itakayoangazia tabia ya mfumo wa kudhibiti ndege kutokana na makosa yanayojitokeza katika sensa.
Pia siku ya Jumapili kulifanyika sherehe za kuwapatia heshima zao za mwisho waathiriwa.
Maelfu ya watu walikongamana katika kanisa la Holy Trinity Cathedral mjini Addis Ababa ambapo majeneza yalivikwa bendera ya kitaifa.
Hakuna mwili uliotambulika kutokana na ajali hiyo.
Je tunajua nini kuhusu ajali hiyo ya kampuni ya ndege ya Ethiopia?
Ndege ya Ethiopia Airline 302 iliondoka kutoka uwanja wa kimataifa wa Addis Ababa wa Bole asubuhi ya tarehe 10 mwezi Machi ikielekea jijini Nairobi nchini Kenya.
Dakika chache baadaye, rubani wa chombo hicho aliripoti kupata matatizo angani na kutaka kurudi uwanjani.
Hali ya hewa ilikuwa nzuri lakini muangalizi wa safari za ndege alisema kuwa kupaa kwa ndege hiyo kwa kasi kulikumbwa na matatizo.
Shahidi mmoja katika eneo la ajali aliambia BBC kwamba kulikuwa na moto mkubwa baada ya ndege hiyo kuanguka.
Wachunguzi wa usalama wa safari za ndege walichunguza data ya ndege hiyo na sauti iliopo katika eneo la rubani ama kijiboksi cheusi kama kinavyoitwa na kutoa matokeo yao kwa serikali ya Ethiopia.

Je nini kilichotokea nchini Indonesia?

Mnamo tarehe 29 Oktoba ndege aina ya Lion Air Flight 610 ilianguka baada ya kuondoka katika uwanja wa ndege wa Jakarta na kuwaua watu 189.
Familia za waathiriwa zilitembelea eneo la mkasa ili kutoa heshima yao ya mwishoHaki miliki ya pichaREUTERS
Image captionFamilia za waathiriwa zilitembelea eneo la mkasa ili kutoa heshima yao ya mwisho
Wachunguzi baadaye waligundua matatizo ndani ya mfumo wa ndege hiyo ambayo ina uwezo wa kuzuia ndege kuelekea juu ambapo inaweza kupoteza mwinuko wake.
Wakati wa ndege aina ya JT610, mfumo huo ulilazimu pua ya ndege hiyo kuangalia chini wakati ambapo ndege hiyo ilikuwa haina matatizo kutokana na sensa mbaya.
Marubani walijaribu kurekebisha tatizo hilo kwa kuilazimisha pua ya ndege hiyo kuangalia juu hadi mfumo huo ulipoilazimisha kushuka chini .
Kitendo hicho kilifanyika mara 20.
Kufuatia kuanguka kwa mara ya pili kwa ndege hiyo, kampuni za ndege kote duniani zilisimamisha operesheni za ndege aina ya Boeing 737 Max 8 .