IDADI ya watu waliokufa kutokana na mvua kubwa zilizosababisha mafuriko Kusini mwa Malawi imefikia watu 28. Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi hiyo iliyotolewa Jumamosi imesema kuwa wakati huohuo idadi ya walioathirika inakadiriwa kuongezeka mara dufu.


Msemaji wa Wizara hiyo anayehusika na udhibiti wa maafa, Chipiliro Khamula, amesema watu 124 wamejeruhiwa huku takribani wengine zaidi ya 200,000 wamelazimika kuhama makazi yao katika jumla ya wilaya 14.
Wakati huohuo Rais wa Malawi, Arthur Peter Mutharika ametangaza tukio hilo kuwa janga la kitaifa baada ya dhoruba kali kusababisha kuta za mito kubomoka na mafuriko kufunika vijiji hivyo.
Katika maeneo hayo umeme umekatika na huduma ya maji inakosekana.
Rais Mutharika ameelekeza misaada ya dharura kupelekwa katika maeneo hayo yaliyoathirika na kuratibiwa kwa haraka ikiwemo kulitaka Jeshi la Malawi kusaidia katika zoezi la uokoaji.  
Dhoruba kama hiyo pia imesababisha mafuriko katika baadhi ya mikoa nchini Msumbiji.