Timu ya taifa-Taifa Stars, juzi ilikabidhiwa vifaa vya michezo na wadhamini wao kampuni ya Bia ya Serengeti pamoja na Benki ya NMB tayari kwa ajili ya mashindano maalum ya nchi sita Bonde la Mto Nile yatakayoanza wiki ijayo.
Vifaa hivyo vyenye thamani ya shilingi milioni 20 vilikabidhiwa kwa timu hiyo na Afisa Masoko wa NMB Shilla Senkoro.
Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Senkoro alisema NMB ina matumani kwa vifaa hivyo wachezaji watapata hamasa ya kufanya vizuri kwenye mashindano hayo.
"Ni matumaini yetu kwa vifaa hivi kama ilivyo kawaida vitachangia vijana kufanya vizuri kwenye mashindano yaliyopo mbele yao", alisema Senkoro.
Aidha, kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la soka nchini 'TFF' Sunday Kayuni alishukuru kampuni ya SBL pamoja na benki ya NMB kwa vifaa hivyo na kuwataka wachezaji kuwalipa kwa kufanya vizuri kwenye mashindano hayo.
"Kwa niaba ya Kamati ya Utendaji ya TFF, nawashukuru NMB pamoja na Serengeti kwa vifaa hivi ambavyo vitasaidia zaidi vijana wetu kufanya vizuri', alisema Kayuni.
Naye naodha wa Stars, Shedrack Nsajigwa alisema yeye pamoja na wenzake watajituma kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye mashindano hayo.
Vifaa vilivyokabidhiwa kwa timu hiyo ni pamoja na jezi kwa ajili ya mechi, sare kwa ajili ya mazoezi, mabegi, viatu vya mazoezi pamoja na mechi kwa wachezaji wote.
Kundi la kwanza la Stars litakalokuwa na watu tisa linaondoka leo kwenda nchini Misri, wakati kundi lingine la wachezaji litaondoka nchini kesho.