WABUNGE wote wa majimbo ya Mkoa wa Dodoma, wakuu wa wilaya zote na mkuu wa Mkoa wa Dodoma, ni miongoni mwa wageni mashuhuri walioalikwa kuhudhuria shindano la kumpata mrembo wa utalii wa Mkoa wa Dodoma Oktoba 22, 2011.
Mkurugenzi wa Miss Utalii Taifa, Gideon Chipungahelo, alisema jana kwamba shindano hilo limepangwa kufanyika katika ukumbi wa Hoteli ya kitalii ya New Dodoma Hotel, na kushirikisha jumla ya warembo 15 kutoka wilaya zote za Mkoa wa Dodoma.
Alisema warembo hao kwa sasa wanaendelea na kambi ya mazoezi katika Hotel hiyo chini ya mkufunzi wao Neema Isdory, ambaye ni Miss Utalii Njombe 2010/2011 na Tabia Msuta, ambaye ni Miss Utalii Vyuo Vikuu Kanda ya Kati 2010/2011.
Aidha, Mkurugenzi wa Miss Utalii Mkoa wa Dodoma, Charles Gabriel, amewataka wakazi wa Dodoma na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi katika kushuhudia mabinti wa mkoa huo wakionyesha na kutangaza utamaduni, utalii, mitindo na mianya ya uwekezaji ya Mkoa wa Dodoma.
Alisema mpaka sasa wadhamini waliojitokeza ni pamoja na Asante Water, Kifimbo Radio, New Dodoma Hotel, Ngoto Furniture, Royal Village, Clouds FM Radio, TANAPA, Ngorongoro Crater, VETA Hotel, Side Way Lodge, Shabibi Buss Service na Moronga By Makai Enterprises.
Wengine ni pamoja na Kampuni ya Free Media inayochapisha magazeti ya Tanzania Daima na Sayari, Image Masters, Papaa Msofe, Zizzou Fashion, Dar City College, Kumekucha Action Mart, Viovena & Co LTD, pamoja na waheshimiwa wabunge wa Dodoma.