Mwanamke kutoka Ufaransa ametekwa nyara na kundi la watu waliokuwa na silaha karibu na Lamu, Kenya.
Shambulio hilo limetokea majuma matatu tu baada ya watalii wawili kutoka Uingereza kushambuliwa piya huko Kiwayu, kaskazini zaidi ya mwambao wa Kenya.
Wanaume waliokuwa na silaha walimpiga risasi mwanamume wa Kingereza na kumteka nyara mkewe, ambaye anafikiriwa anazuwiliwa nchini Somalia.
Washambuliaji waliingia usiku wa manane na kumteka mwanamke kutoka Ufaransa aliyekuwa kakodi nyumba Ras Kitau.

Milio ya risasi ilisikika upande wa pili wa Lamu, katika kisiwa cha Shela.
Mwanamke huyo ambaye anafikiriwa kuwa mlemavu, alikimbizwa kwenye boti.
Polisi wa Kenya wanaripotiwa na shirika la habari la AFP, wakisema wametuma boti ya kasi kwenda kuwaandama watekaji nyara, ambao wanashukiwa wanaelekea Somalia.
Majuma matatu yaliyopita watalii wawili kutoka Uingereza, David na Judith Tebbutt, walishambuliwa kaskazini zaidi ya mwambao wa Kenya, karibu na mpaka wa Somalia.
Bwana Tebbutt alipigwa risasi na kuuliwa na gengi hilo.
Judith Tebbutt anazuwiliwa nchini Somalia.
Utekaji nyara wa jana usiku umefanywa katika eneo lisilokuwa mbali, na linaweza kuchafua sana sekta ya utalii huko Lamu, sekta ambayo inategemewa na wengi.