NYUMBA ya watu mashuhuri haikaukiwi habari na kila kukicha heri ya jana kuliko ya leo! Inadaiwa kuwa hali si shwari katika nyumba wanayoishi mastaa wawili wa Kibongo, Wema Isaac Sepetu na Naseeb Abdul Jumaa ‘Diamond’, Ijumaa linafunguka.

Chanzo cha karibu na mastaa hao kinadai kuwa, katika korido za nyumba hiyo wanayoishi maeneo ya Sinza-Madukani, Dar es Salaam, Wema na mama mzazi wa Diamond, Sanura Khassim ‘Sandra’ ni mwendo wa vikumbo, vituko na mafumbo ya hapa na pale.

ISHU ILIANZA WEMA NA DIAMOND WALIPORUDIANA
Chanzo hicho cha ndani kilidai kuwa, kumekuwa na hali ya kutoelewana kati ya Wema na mama mkwe wake huyo tangu mnyange huyo aliporudiana na ‘baby’ wake Diamond ambapo alirejea kwa mara nyingine ndani ya nyumba hiyo.


Inadaiwa kuwa, siku Wema aliyorejesha ‘majeshi’ mjengoni hapo, mama Diamond hakuwepo, lakini alipoibuka akakuta viatu vya mlimbwende huyo mlangoni, eti ikadaiwa kuwa alianza kurusha kijembe huku akihoji uwepo wake.
“Asikwambie mtu, huku kimenuka, siku iliyofuata vikumbo, vituko, vijembe na mafumbo vilizidi kutawala hadi Wema akapandwa na hasira za Kinyamwezi, lakini hakuwa na la kufanya,” kilisema chanzo chetu.

WEMA WA MACHOZI
Ilidaiwa kuwa kufuatia hali hiyo, Wema amekuwa akimwaga machozi ‘deile’ baada ya kujaribu kujibu mapigo ikashindikana.
TUKIO LA KUKUMBUKWA


Chanzo kilidai kuwa tukio la kukumbukwa lililoingia kwenye historia ya mapenzi ya wawili hao ni lile la mama Diamond kugonga chumba cha mwanaye asubuhi huku wakiwa wamelala.
Ilidaiwa kuwa, mzazi huyo alifanya hivyo kumkumbusha Diamond kuwahi mahakamani kwa ajili ya kesi ya madai inayomkabili Mahakama Kuu.

MISHEMISHE ZINAENDELEA
Chanzo kiliendelea kudai kuwa, huo ni mwendelezo wa mishemishe hizo ambazo zilikuwepo hata kabla ya Diamond kummwaga Wema, lakini waliporudiana ndipo hali ya hewa ikawa imechafuka zaidi.

WAWEKWA KIKAO
Ilidaiwa kuwa kutokana na sekeseke hilo, kiliwekwa kikao ili kuweka mambo sawa, lakini hakuna kilichorekebishika kwani kila mmoja alikuwa aking’ang’ania kuombwa msamaha.

WEMA ANASEMAJE?
Kama kawa, kama dawa, ili kupata mzani wa habari hiyo, Ijumaa lilimuinulia Wema mkonga wa simu na kumpa za uso ‘laivu’ kuhusu ishu hiyo ambapo hakutaka kuingia kiundani kwa madai kuwa hayo ni maisha yake na haoni sababu ya kuyaanika.

Mama Diamond je?
Jitihada za kumpata mama Diamond kuzungumzia ishu hiyo hazikuzaa matunda baada ya simu yake kutopatikana.
DIAMOND AFUNGUKA
Diamond alipopigiwa simu na paparazi wetu na kuulizwa juu ya madai hayo alisema:
“Dah! Mkubwa huwa sipendi mambo hayo yaandikwe gazetini.”