ELIZABETH Michael ‘Lulu’ na kichwa cha Bongo Fleva, Ali Saleh Kiba ‘Alikiba’, wamebananishwa kwa nyakati tofauti na kujikuta wakibumburua siri ya penzi lao huku kila mmoja akimuona mwenzake zilipendwa, Ijumaa Wikienda linafunguka.

Lulu ndiye aliyeanza kutoa siri alipofunua kinywa hivi karibuni ndani ya Viwanja vya Leaders, Kinondoni jijini Dar es Salaam baada ya ‘Vuvuzela’ wetu kumtaka azungumzie penzi lake na Alikiba ambapo bila simile, ‘kichaa’ huyo wa muvi za Kibongo alisema kuwa alishasahau kama aliwahi ‘kutoka’ na msanii huyo kwani kwa sasa siyo siri hisia zake za kimapenzi zipo kwa kinda wa muziki anayefanya vyema katika ardhi ya Obama, Justin Bieber.

Kwa mara ya kwanza, ‘chakaramu’ huyo alikiri kutoka na Alikiba tofauti na siku za nyuma ambapo jambo hilo lilikuwa siri kubwa na hakuwa tayari kulizungumzia.

Alifunguka: “Duh! Umenikumbusha mbali sana. Nilishasahau kabisa kama niliwahi kutoka naye. Pamoja na kwamba ni kweli alikuwa mtu wangu, lakini kwa sasa moyo wangu hautaki kusikia kingine zaidi ya Bieber na namuonea wivu sana Selena Gomez (mpenzi wa Bieber).”
Ili kuweka sawa mzani wa habari hiyo, The Biggest IQ Paper, Ijumaa Wikienda lilimtafuta Alikiba ili kusikia anasema nini ambapo naye bila hiyana akatia neno.

“Sina muda na Lulu kwa sasa, kama ni mapenzi yalikuwa zamani, hata mimi nina mambo yangu muhimu na si Lulu,” alisema Alikiba.

Penzi la wawili hao liliwahi kuvuma kwa kasi ya kimbunga na kuripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari, lakini kinachoonekana kwa sasa hawako ‘klozi kiivo’.