Shirikisho moja mashuhuri la matibabu ya watoto nchini Marekani, limesema kuwa hatua ya kuwatahiri watoto wavulana kunaleta faida kubwa zaidi za kiafya kuliko tisho kwa afya ya watoto hao wakati wa upashaji tohara.
Shirikisho la madaktari wa watoto nchini humo, limesema kuwa matokeo ya utafiti wao yameonyesha kuwa kitendo hicho kinasaidia kupunguza uwezekano wa watoto kuugua saratani ya sehemu za mkojo, pamoja na maambukizi ya HIV.
Taarifa hii ya shirikisho hilo ni kinyume na taarifa waliyoitoa miaka kumi na tatu iliyopita ambayo haikueleza faida hizi pamoja na kukosa kuchukua msimamo wowote.
Nchi kadhaa za afrika zimeweza kuunga mkono upashaji tohara kwa wanaume kama njia ya kupunguza maambukizi ya virusi vya HIV.
Pamoja na hilo, wabunge zaidi ya ishirini wa Zimbabwe walitahiriwa mwezi Juni kama sehemu ya kampeini hiyo.