MKUU WA JESHI LA POLISI TANZANIA (IGP) SAID.A.MWEMA AKITOA TAARIFA YA KIFO CHA ALIYEKUWA KAMANDA WA POLISI MKOA WA MWANZA KAMISHINA MSAIDIZI WA POLISI (ACP) LIBERATUS BARLOW KILICHOSABABISHWA NA KUPIGWA RISASI ENEO LA KITANGIRI MKOANI MWANZA. KULIA NI KAMISHINA WA OPERESHENI WA JESHI LA POLISI CP. PAUL CHAGONJA.( PICHA NA OFISI YA MSEMAJI WA POLISI.)
Napenda kutumia fursa hii kuwapa taarifa kuhusu tukio la mauaji ya aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Kamishina Msaidizi wa Polisi Liberatus Barlow yaliyofanywa na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi usiku wa kuamkia leo tarehe 13/10/2012 majira ya saa saba usiku Mkoani Mwanza.

Tukio hilo limetokea wakati kamanda huyo akitokea kwenye kikao cha harusi ya ndugu yake eneo la Frolida hotel Mwanza mjini, akiwa na ndugu yake waliyeongozana nae kutoka kwenye kikao hicho.

Wakati akimshusha huyo ndugu yake eneo la Kitangiri Minazi Mitatu, walitokea watu wanaosadikika kuwa ni majambazi, na kumvamia na kuanza kumshambulia kwa risasi na kumuua papohapo.


 Ndugu wananchi, kufuatia tukio hilo, tayari nimemtuma Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai DCI Robert Manumba kwenda mkoani Mwanza kwa lengo la kuimarisha ulinzi na upepelezi wa tukio hilo.


Najua tukio hili limetushitua na kutuhuzunisha wote. Hivyo, wakati tukiendelea na taratibu zingine kuhusiana na tukio hilo, niwaombe wananchi wote kuwa watulivu na kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi, utakaowezesha kuwabaini wahalifu hao.

 Tutaendelea kuwapa taarifa za tukio hilo, kadri tutakavyoendelea kuzipata.