Rais wa Ufaransa Francois Hollande, amesema nchi yake iko tayari kusaidia jeshi la Mali kupambana na waasi wanaodhibiti Kaskazini mwa nchi.
Amesema kuwa ataweza kujibu haraka ombi kwa serikali yake la kutoa msaada wa kijeshi kwa nchi hiyo ili kusitisha harakati za wapiganaji hao.
Lakini alisema kuwa wataweza tu kufanya kazi yao ikiwa Umoja wa Mataifa utawaidhinisha. Umoja wa Matifa hata hivyo ndio umetoa wito wa kupelekwa kwa wanajeshi wa kimataifa nchini humo katika mkutano wa dharura wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa.
Rais Hollande, alisema kuwa harakati za wapigajani hao wanaohusishwa na kundi la Al Qaeda,sasa zinatishia utahbiti wa Mali. Hadi sasa Ufaransa imesema iko tayari tu kutoa mafunzo kwa jeshi la Mali.

Awali baraza la usalama la Umoja wa mataifa lilitoa wito wa kupelekwa kwa wanajeshi wa kimataifa nchini humo ambako wapiganaji wa kiisilamu wanadai wameuteka mji muhimu wa Konna.
Wakati huohuo, duru za kidiplomasia zinasema kuwa rais wa nchi hiyo ametoa wito kwa Ufaransa kusaidia katika kupambana na wapiganaji hao, hoja iliyojadiliwa katika mkutano wa dharura wa baraza la usalama la umoja wa mataifa.
Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Susan Rice, alihoji ikiwa rais Dioncounda Traore alikuwa ametoa ombi maalum na kufafanua aina ya msaada anaotaka.
Mwezi jana Umoja wa Mataifa uliidhinisha mpango wa kutuma wanajeshi elfu tatu kuweza kutwaa eneo la Kaskazini mwa nchi ambalo linadhibitiwa na makundi ya kigaidi yaliyo na uhusiano na kundi la Al Qaeda.
Wapiganaji wa kiisilamu wameweka sheria kali za kiisilamu katika eneo hilo.
Kwa sababu ya mipango ya usafiri na vifaa , kikosi cha wanajeshi wa Afrika hakitatarajiwa kuanza kazi hadi ifikapo Septemba au Oktoba.