MAFURIKO YAZAMISHA NYUMBA NA KUWANASA WATOTO 2 NCHINI KENYA

Polisi nchini Kenya wameelezea BBC kuwa watoto 2 wamekwama nyumbani kwao baada ya kufukiwa na tope na maji yaliyosababisha maporomoko ya ardhi.

Watoto hao walikuwa wamelala katika kijiji cha Narok kilomita kadhaa kutoka mji wa Nairobi, mvua kubwa iliponyesha na kusababisha maji kusomba majumba kadhaa katika mtaa wao.
Shirika la msalaba mwekundu nchini Kenya limeonya watu wanaoishi maeneo yanayotishiwa kukumbwa na mafuriko wahamie sehemu za juu na milima.

Mvua kubwa imekuwa ikinyesha katika sehemu nyingi nchini humo na inaaminiwa kuendelea kunyesha.

Katibu mkuu wa shirika hilo nchini Kenya Abbas Gulet ameambia BBC kuwa maeneo yaliyoahiriwa zaidi ni pamoja na Nairobi na maeneo yaliyo pembezoni, na garissa ambapo watu kadhaa wamefukiwa na maporomoko ya ardhi au kuzingirwa na maji.

Maafa makubwa


Kufikia sasa watu 36 wamefariki kutokana na mafuriko hayo yaliyoanza chini ya mwezi mmoja.

Kawaida msimu wa mvua nchini Kenya huwa kati ya mwezi Machi na May, lakini wadadisi wanasema kuwa safari hii mvua imenyesha kwa wingi zaidi.