WAREMBO waliojitokeza kushiriki kinyang'anyiro cha kuwania taji la kitongoji cha Kigamboni mwaka huu "Redd's Miss Kigamboni 2013" wanatarajiwa kuanza kambi yao leo Jumatatu kwenye ukumbi wa Break Point, Posta jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na Globu ya Jamii, Mratibu wa shindano hilo, wa kampuni ya K& L Media Solutions, Somoe Ng'itu, alisema kuwa maandalizi ya shindano hilo yanaendelea na bado nafasi iko wazi kwa wasichana wote wenye sifa za kushiriki shindano hilo kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini.

Somoe alisema kwamba lengo la kuweka wazi na kuwahamasisha warembo ni kutaka kutoa nafasi kwa wasichana wengi zaidi kujiandikisha na hatimaye kupata mshindi atakayekiwakilisha vyema kitongoji hicho katika mashindano ya ngazi ya Kanda yatakayofanyika baadae mwezi ujao.
"Tuko katika hatua za mwisho katika kuandaa shindano hili na kamati imejipanga kuhakikisha shindano linafanyika kwa ubora na hatimaye kuendelea kutetea taji la Miss Temeke," alisema Somoe.
Aliongeza kwamba fomu kwa ajili ya kushiriki shindano hilo zinapatikana bure na washiriki ambao wako tayari wanaombwa kufika katika mazoezi hayo ambayo yatakuwa chini ya Blessing Ngowi, ambaye alishiriki fainali za Miss Tanzania mwaka juzi na ndiye mrembo wa taifa wa Kanda ya Elimu ya Juu mwaka huo.
Alisema pia makampuni na taasisi mbalimbali zinakaribishwa kudhamini shindano hilo ambalo mwaka jana lilitoa mshindi katika kinyang'anyiro cha Kanda ya Temeke ambaye ni Edda Sylivester.

Edda alifanikiwa kushika nafasi ya tatu kwenye fainali za taifa huku mshindi wa taifa ni Brigitte Alfred ambaye mwaka huu ataenda kupeperusha bendera ya nchi katika mashindano ya dunia.