HATIMAYE mabingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom, Yanga, wamemtambulisha rasmi nyota wao wa zamani, Mrisho Ngasa, aliyekuwa akiwatumikia watani wao, Simba, msimu huu wa ligi uliomalizika mwishoni mwa wiki.
Kabla ya kutua Simba kwa mkopo katika usajili wa dirisha dogo, Ngasa alitokea Azam FC ambayo nayo ilimtoa Yanga kwa mbwembwe, kabla ya kulikoroga baada ya kuibusu jezi ya Yanga wakati Azam ilipocheza na AS Vita ya DRC wakati wa michuano ya Kagame Cup, mwaka jana.
Akizungumza wakati wa utambulisho wa nyota huyo aliyeziteka hisia za mashabiki wa Yanga waliofurika makao makuu ya klabu hiyo Jangwani jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Lawrence Mwalusako, alisema wameamua kumtambulisha nyota huyo baada ya kuhakikisha wamemaliza kila taratibu za usajili.
Naye Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, Abdallah Ahmad Binkleb, alisema Ngassa ametua Jangwani kwa mkataba wa miaka miwili na ataanza kazi kwenye mashindano ya Kagame yanayotarajiwa kuanza hivi karibuni nchini Sudan na kudai kuwa watani wao Simba kumpatia gari ilikuwa ni ushawishi ili waweze kumpata.
Binkleb alisema, walianza mazungumzo na Ngasa miezi sita iliyopita hadi kuja kumtambulisha na kufafanua kuwa wamemkabidhi jezi yenye jina lake bila namba kutokana na zoezi la usajili kuwa bado linaendelea.
“Ngasa ni mchezaji halali wa Yanga kuanzia leo, amesaini mkataba wa miaka miwili na tumehakikisha tunafuata taratibu zote za usajili,” alisema Binkleb.
Akizungumzia kurejea kwake Jangwani, Ngasa alisema hajakurupuka kwa kuwa ni mapenzi yake toka zamani na alikuwa hajisikii vizuri alipokuwa Azam FC na Simba.
Aliongeza kuwa Simba ni waongo kwani hawakuingia naye mkataba walipomchukua Azam kwa mkopo.
“Mimi Yanga ndiyo timu ambayo ninaipenda kuichezea na namshukuru Mungu pamoja na viongozi wa Yanga kwa kufanikisha mpaka nimerejea katika klabu ambayo ninaipenda miaka yote, pia nawashukuru mashabiki waliokuwa wananisapoti nikiwa Azam na Simba mpaka narudi nyumbani, nawaomba waendelee kunisapoti,” alisema na kuongeza: “Simba walionekana kukosa imani na mimi kwa kuwa nilionyesha wazi kuipenda Yanga, ila ilikuwa sio kweli na kwa kuwa wao walikosa imani na mimi, ndiyo walizidisha nizidi kuipenda Yanga na nimerudi, ila kusema nilisaini Simba sio kweli, kwanza nilikuwa na mkataba na Azam ambao walinipeleka kwa mkopo Simba,” alisema Ngasa.
Katika hatua nyingine, habari kutoka ndani ya Yanga, zinaeleza kuwa zoezi la mwenyekiti wa klabu hiyo, Yusuf Manji kuwapa vitita vyao benchi la ufundi na wachezaji baada ya kutwaa ubingwa wa bara, jana lilikwama kutokana na bosi huyo kushindwa kurejea nchini kama