Mabingwa wa Ligi Kuu nchini England, Manchester United wametangaza kwamba, Sir Alex Ferguson atastaafu kama meneja wa klabu hiyo mwishoni mwa msimu huu.Sir Alex anatajwa kuwa ndiye meneja mwenye mafanikio makubwa katika historia ya soka la Uingereza.

Tangu alipojiunga na klabu hiyo mnamo mwaka 1986, ameshinda mataji mawili ya Klabu Bingwa Barani Ulaya, mataji kumi na tatu ya Ligi Kuu ya England na Kombe la FA mara tano.

Katika taarifa yake, Sir Alex amesema ni muda muafaka kwake kustaafu wakati klabu ikiwa imejizatiti katika nafasi nzuri.

Ferguson atabakia Manchester United kama mmoja wa wakurugenzi na balozi.

Watu mbalimbali wamekuwa wakitoa salamu za kumtakia kheri, miongoni mwao akiwemo Waziri Mkuu wa Uingereza,David Cameron na wanasiasa mbalimbali pamoja na mashabiki na wachezaji wa zamani wa Uingereza na Manchester United.

Hofu imetanda miongoni mwa mashabiki wa Manchester United ambao wamekuwa wakijiuliza maisha yatakuwaje bila ya Sir Alex Ferguson kwenye klabu hiyo yenye mashabiki wengi Ulimwenguni.