Mabasi yakiwa yameegeshwa kwenye Stendi Kuu ya Mabasi yaendayo mikoani Ubungo jijini Dar es Salaam. Picha ya Maktaba
Dar es Salaam.
Hali ya usalama kwenye Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo Mikoani (UBT), imekuwa tete baada ya kuibuka kwa kundi kubwa la matapeli wanaowaibia abiria na kuwabambikizia kesi kwa kutumia njia ya ulinzi shirikishi.
Mbali na kufanyika kwa vitendo hivyo kituo hicho kinadaiwa kuwa soko kubwa la biashara haramu ya dawa za kulevya aina ya Bangi na Mirungi.
Kundi hilo ambalo linajulikana kama vishoka limekuwa likifanya vitendo hivyo kuanzia saa mbili usiku kwa kujifanya kuwa wao ulinzi shirikishi, na kufanya utapeli huo kwa kuwakamata abiria na baadhi ya watu wanaoingia kwenye kituo hicho na kuwapa makosa mbalimbali.
Uchunguzi uliyofanywa na gazeti hili takriban siku tatu kwenye kituo hicho majira usiku na mchana, umebaini kwamba mchezo huo mchafu umekuwa ukifanyika kwa muda mrefu ambapo tayari kundi kubwa la watu wametapeliwa na kuibiwa vitu mbalimbali.
Uchunguzi huo umebaini kwamba moja ya utapeli unaofanywa na kundi hilo la vijana wanaojiita ulinzi shirikishi, ni kutumia pete feki za dhahabu ambazo wanazitumia kuwatapeli fedha abiria.
Pia, licha ya kufanya utapeli huo kwa kutumia dhahabu feki, kundi hilo linatumia bidhaa ya sabuni kuwatapeli simu abiria. Sabuni hutengenezwa kwa mfano wa simu na kuwabambika watu kuwa ni simu halisi.
Licha ya kufanyika kwa vitendo hivyo, uchunguzi pia umebaini kuwepo kwa biashara haramu ya dawa za kulevya aina ya bangi na mirungi.
Uchunguzi pia umebaini kwamba vijana hao matapeli wakimkamata mtu kwa kisingizio cha kuhusika na wizi, wanamtoza faini kati ya Sh50,000 hadi 70,000. Makosa yanayodaiwa kuwa madogo kama kukojoa au kutupa uchafu wanatoza faini ya kati ya Sh10,000 hadi Sh20,000 kila siku.
Akizungumzia suala hilo Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Ubungo (NHC), Amani Sizia alithibitisha kuwepo kwa vitendo hivyo vya uhalifu na kudai kwamba UBT imegeuka kuwa shamba la bibi kwa wahalifu.
Sizia alisema: “Kwa kweli hali ya kituo cha mabasi ya Ubungo na maeneo jirani imekuwa mbaya sana, kuna vikundi vya ulinzi shirikishi ambavyo ni feki zaidi ya vitano. Vikundi hivyo vimekuwa vikifanya kazi ya kuwatapeli abiria.”
Alisema kwa kuthibitisha zaidi nyakati za usiku kila kibaka anageuka kuwa mlinzi shirikishi, na kufanya kazi ya utapeli ili kujipatia fedha.
“Nashukuru sana ndugu yangu mwandishi kwa kunitafuta UBT kwa sasa haifai, kuna vitendo vingi vya uhalifu ambavyo vinafanyika nyakati za usiku. Kila kibaka ikifika wakati huo anageuka kuwa mlinzi shirikishi,” alisema Sizia Sizia alibainisha kwamba ukitaka kuamini matapeli hao wanafanya kazi hiyo bila kuwa na vitambulisho, ni kwamba wanachofanya ni kuwakamata watu na kuwaomba fedha bila hata kuwafikisha kwenye ofisi za kata. Mwandishi wa habali hizi alithibitisha kuwepo kwa matapeli hao baada ya kusimama sehemu moja ya eneo hilo la Ubungo na kujisaidia haja ndogo, ambapo alikuja kijana mmoja aliyejitambulisha kuwa ni mlinzi shirikishi na kumtaka alipe fedha.
Mwandishi alipomtaka kijana huyo aliyevalia kofia na koti lenye rangi ya kung’aa, hakuwa nacho na kulazimisha alipwe fedha ili amwachie.
Mwandishi alimpa Sh2,000 na kumwachia huku amkimtaka asirudie tena kufanya kosa hilo.
Gazeti hili lilimtafuta Kamanda wa Ulinzi Shirikishi kituoni hapo James Mapunda, ambaye alithibitisha kuwapo kwa vitendo hivyo vya kihalifu na kudai kuwa vinafanywa na watu wanaojitambulisha kama walinzi jamii.
Kamanda huyo alikwenda mbali zaidi na kubainisha kuwa licha ya kufanyika kwa uhalifu huo pia kuna vitendo vingine vya biashara haramu ya bangi, dawa za kulevya aina ya mirungi, wizi wa kompyuta mpakato (laptop) pamoja na biashara ya tiketi bandia.
“Ndugu yangu mwandishi hapa hapafai hata kidogo kwani imegeuka kambi ya matapeli na wezi kwani kumekuwa na vitendo vingi vya kihalifu vinavyofanywa na wahalifu wanaojitambulisha kama walinzi shirikishi. Hata hivyo kumekuwa kunafanyika biashara haramu ya dawa za kulevya,” alisema Mapunda.
Mapunda alidai kwamba vitendo hivyo vinafanyika na kwamba haviwezi kuisha kwani kuna baadhi ya maofisa wa polisi kituoni hapo wanatambua, kwani huwa wanalipwa posho na watu hao.
Gazeti hili lilimtafuta Kamanda wa Polisi Magomeni (OCD) Yahaya Athumani ili kuthibitisha vitendo hivyo, hata hivyo alisema hana taarifa za kufanyika kwa utapeli huo na biashara haramu ya dawa za kulevya.
“Tunatambua kwamba UBT kuna uhalifu mwingi ambao unafanyika, lakini tumekuwa tukifanya doria za mara kwa mara ili kuimarisha ulinzi,” alisema Athumani.
Kamanda Athumani alikana kuwa na taarifa za kufanyika kwa vitendo hivyo na kuahidi kufanyia kazi taarifa hizo.
“Ndugu yangu wewe ndiyo unanipa taarifa, kwa kuwa mimi siyo msemaji wa Polisi nitafanyia kazi, kwani UBT ipo chini yangu,”alisema.
Hata hivyo gazeti hili lina taarifa za kuwepo kwa Polisi wanaoshirikiana na wahalifu hao kwa kulipwa posho kila wanapo fanya vitendo hivyo.