Mchambuzi wa masuala ya siasa na Mhadhiri wa UDSM, Dk Benson Bana 
Dar es Salaam. Siku moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kusema dawa ya kudai Katiba Mpya haitafanikiwa kwa maandamano na vurugu huku akipendekeza itumike njia ya mazungumzo na kukubaliana kwa pamoja, wasomi nchini wamevitaka vyama vya upinzani kutumia busara na kukubali ushauri huo.
Oktoba 10 mwaka huu, viongozi wakuu wa vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na CUF wamepanga kufanya maandamano nchi nzima kupinga Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa 2013, uliopitishwa wakati wa mkutano wa 12 wa Bunge mwezi uliopita kwa maelezo kuwa una kasoro.
Katika hotuba yake ya kila mwezi kwa wananchi aliyoitoa juzi,
Rais Kikwete alisema kuandamana nchi nzima au kuchukua hatua za kutokutii sheria kama Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe anavyotaka hakutaleta mabadiliko wanayoyataka katika sheria hiyo.
Alishauri utumike utaratibu kama ule wa mwaka 2012, ambapo baada ya kuibuka kwa mazingira ya kutokuelewana katika suala la katiba, pande zote zilikaa pamoja na kuzungumzia hoja moja baada ya nyingine na kukubaliana nini kifanyike na baada ya kuridhiana hatua zipasavyo za kisheria na kanuni zilichukuliwa na kumaliza mzozo.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti leo, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Profesa Gaudence Mpangala alisema ni jambo la busara kwa Rais Kikwete kuonyesha kutaka suluhu katika mvutano uliopo sasa.
“Najua wazi kuwa ni vigumu kwa Rais kukubaliana na wapinzani, lakini kitendo cha kuonyesha nia ya kutaka kukutana nao na kuweka mambo sawa kinaleta ishara nzuri,” alisema na kuongeza:
“Binafsi natambua kuna mambo hayakwenda sawa katika upitishwaji wa muswada ule, lakini hilo linaweza kumalizwa kama pande zote zikikutana, wapinzani wajaribu kutafakari kuhusu jambo hili.”
Naye Bashiru Ali alisema: “Inategemea…, sijui kama wanasiasa wataamini kauli iliyotolewa na Rais Kikwete, lakini wanatakiwa kutambua kuwa Rais ameonyesha nia ya dhati na hekima ya kutaka kuweka pembeni tofauti zilizopo sasa.”
Aliongeza: “Nakubaliana na Rais kwamba mchakato wa kupata Katiba Mpya hauwezi kufanikiwa kama malumbano yaliyopo sasa yataendelea. Wanasiasa waonyeshe dhamira kwa kuweka masilahi ya taifa mbele, lakini wakikaidi na kuendelea na mipango yao wataharibu mchakato mzima.”
Kwa upande wake Profesa Chris Peter Maina ambaye yupo nchini Ujerumani, alisema hotuba ya Rais imetoa msimamo wake kuhusu mchakato wa Katiba Mpya, “Kitendo cha yeye kukubali kuzungumza na wapinzani  ni kizuri na kitaleta suluhu ya kudumu.”
Mchambuzi wa masuala ya siasa na mhadhiri wa UDSM, Dk Benson Bana alisema hotuba hiyo imeonyesha wazi kuwa Rais Kikwete bado hajapwaya katika uongozi.“Ni wazi kuwa vyama vya siasa vinaingilia mchakato wa Katiba na Rais amelizungumza hilo wazi, wanasiasa wetu baadhi wameonyesha unafiki. Wanasiasa hasa wapinzani wafuate ushauri wake kwa kukubali kukaa meza moja na kuzungumza” alisema Dk Bana.