Dk. Sengondo Mvungi.
MJUMBE wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ambaye pia ni Mhadhiri Mwandamzi wa Sheria wa Chuo Kikuu cha Bagamayo (UB), Dk. Sengondo Mvungi, usiku wa kuamkia leo amevamiwa na watu wasiyojulikana na kukatwa mapanga maeneo mbalimbali mwilini ikiwemo sehemu za kichwani kwa madai ya kutaka wapatie fedha. Watu hao walitimiza lengo lao hilo baada ya Dk. Mvungi kuwaambia hana fedha ndipo walipoanza kumcharanga mapanga.
Mtoto mkubwa wa Dk. Mvungi aitwaye Dk. Natujwa Mvungi ameeleza kuwa baada ya watu hao kumjeruhi baba yake na kufanikiwa kuondoka, walimchukua na kumkimbiza katika Hospitali ya Tumbi mkoani Pwani ambapo amepatiwa huduma ya kwanza kisha kumkimbiza katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo baadaye alipelekwa kwenye wodi katika Taasisi ya Mifupa (MOI) kwa ajili ya matibabu.
Dk. Mvungi aliwahi kugombea urais katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 2005 kwa tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi.