Wakati Tanesco ikitakiwa kulipa deni hilo la Sh884.5 bilioni, mapato yake kwa mujibu wa bajeti ya 2012/2013, ni kati ya Sh60 bilioni na Sh70 bilioni kwa mwezi, huku matumizi yake yakiwa Sh11 bilioni.PICHA|MAKTABA 

Dar es Salaam. 
Wakati Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) likipandisha bei ya umeme kwa zaidi ya asilimia 40, limetakiwa kulipa zaidi ya Sh844.8 bilioni, kwa kampuni zilizoifungulia kesi mbili tofauti kwa kukiuka mkataba wa kukodisha mitambo ya kuzalisha umeme ya Kampuni ya IPTL.
Baada ya shirika hilo kushindwa kesi hiyo, sasa limepoteza pia haki ya kumiliki mitambo ya IPTL ikiwa ni mwaka mmoja tu kabla ya muda wa kuikodisha ufikie kikomo na mitambo hiyo iwe mali ya Tanesco kwa asilimia 100.
Mkataba huo wa kukodisha mitambo hiyo wa miaka 20 ulioingiwa mwaka 1995, ulikuwa ufikie kikomo mwaka 2015.
Kiasi hicho cha fedha ni sawa na kiasi cha fedha ambazo kinapangwa kwa ajili ya bajeti za wizara nyeti nchini.
Wakati Tanesco ikitakiwa kulipa deni hilo la Sh884.5 bilioni, mapato yake kwa mujibu wa bajeti ya 2012/2013, ni kati ya Sh60 bilioni na Sh70 bilioni kwa mwezi, huku matumizi yake yakiwa Sh11 bilioni.
Taarifa ambazo gazeti hili limezipata, zinaeleza kuwa Tanesco ilikuwa na kesi mbili, moja iliyofunguliwa jijini Dar es Salaam na nyingine Washington DC nchini Marekani.
Kwa upande wa kesi ya jijini Dar es Salaam, hukumu yake ilitolewa na Jaji John Utamwa wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Januari 17 mwaka 2014 saa 8:30 usiku.
Hukumu hiyo imeanza kuzua maswali mengi kiwa baadhi ya watu wakihoji kwa nini itolewe usiku na siyo mchana.
Hukumu nyingine ni ile iliyotolewa Februari 12 mwaka 2014 na Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi wa Migogoro ya Uwekezaji cha Washington DC nchini Marekani.
Katika kesi ya jijini Dar es Salaam, mdai alikuwa ni VIP Engineering and Marketing LMT pamoja na Independent Power Tanzania (IPT).
Wajibu madai katika kesi hiyo walikuwa ni Pan Africa Power Solutions T (LTD), Benki Kuu ya Tanzania ambako Tanesco walikuwa wamefungua akaunti maalumu (ESCROW Account), Stanbic Tanzania Ltd pamoja na UBL Bank Tanzania LTD.
Kwenye kesi ya Washington, Standard Charted Bank (Hong Kong) Limited, iliishtaki Tanesco kwa kukiuka mkataba wa kushindwa kuwalipa ushuru wa Dola za Marekani 2.5 milioni kila mwezi.Fedha hizo zinatokana na benki hiyo kununua madeni ya Kampuni ya IPTL, iliyokopa katika Benki mbalimbali za Malaysia.
Baada ya hukumu hizo, fedha ambazo Tanesco ilikuwa ikiziweka kwenye Akaunti Maalumu kwenye Benki Kuu ya Tanzania (ESCROW Account) ambazo zilikuwa zimefikia Dola za Marekani 270 milioni (Sh432 bilioni), zimechukuliwa na Pan Africa Power Solutions T Ltd ambayo pia kwa sasa inamiliki mitambo ya IPTL kwa asilimia 100.
Pia kwenye kesi ya kukiuka masharti ya mkataba ya kushindwa kuwalipa kwa wakati fedha ambazo walikuwa wanadaiwa. Katika hukumu hiyo iliyotolewa Washington, Tanesco imetakiwa kuilipa Standard Charted Bank (Hong Kong) Limited Dola za Marekani 258 milioni sawa na Sh412.8 bilioni.
Hukumu hiyo ilielekeza kuwa, VIP ilipwe Dola za Marekani 67,500,000 sawa na Sh109.1 bilioni, fedha ambazo tayari zimeshalipwa.
Mmiliki wa Kampuni ya VIP
Mmiliki wa Kampuni ya VIP, James Rugemarila alikiri kuuza asilimia 30 ya hisa zake ilizokuwa nazo IPTL, ingawa hakuwa tayari kutoa maelezo zaidi akisema yatatolewa na mwanasheria wake.
“Maswali yako ni ya kisheria zaidi, labda mwanasheria wangu wiki ijayo atatoa ufafanuzi zaidi, kwa sasa hayupo. Ninachoweza kusema ni kweli tumeuza hisa zetu,” alisema Rugemalila.
Jaji Kiongozi, Jundu
Naye Jaji Kiongozi, Fakihi Jundu alisema kuwa hawezi kuthibitisha moja kwa moja kuwa hukumu ya kesi hiyo ilitolewa usiku.
“Sina uhakika kama hukumu hiyo ilitolewa usiku, lakini mahakama kutoa hukumu baada ya jua kuzama siyo mara ya kwanza, kuna wakati mtu alikuja kufungua kesi akitaka Rais asiapishwe, hukumu ile ilitolewa usiku,” alisema Jundu.
Wizara wazungumza
Mkurugenzi wa Tanesco Felchesmi Mramba alitafutwa kupitia simu zake za mkononi, lakini zilikuwa zikiita bila kupokelewa.Msemaji wa Wizara ya Nishati na Madini, Badra Masoud alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, alisema wizara itatoa ufafanuzi huo kesho.
Mazungumzo juu ya uwekezaji wa IPTL nchini yalianza mwaka 1994 na makubaliano kufikiwa mwaka 1995.
Mkataba huo ulikuwa wa miaka 20 ambapo kufikia 2015, mitambo hiyo ilitakiwa kuwa mali ya Tanesco.
Kampuni ya Mechmar kutoka Malaysia ilikuwa ikimiliki mitambo hiyo ya IPTL kwa asilimia 70 huku VIP ikiwa na asilimia 30.
Hivi karibuni Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), ilisema Tanesco ina deni la Sh456.7 bilioni na kampuni mbalimbali ambazo zinazalisha umeme na kuliuzia shirika hilo.