Jeshi la wanamaji nchini Italia , limepata maiti 30 katika mashua ya uvuvi ambayo ilikuwa imewabeba mamia ya wahamiaji haramu.

Mashua hiyo ilipatikana katika eneo moja lililo kati ya mji wa Siciliy nchini Italia na Kaskazini mwa pwani ya Afrika.Wahamiaji waliofariki walisemekana kufariki kutokana na kukosa hewa.
Ugunduzi huo ulifanyika wakati waokoaji walipotumia mashua hiyo kutaka kuokoa idadi kubwa ya watu waliosemekana kuwa katika hali ngumu baharini.
Miongoni mwa watu hao walikuwa wanawake wawili wajawazito.
Wanajeshi hao walisema kuwa mwishoni mwa wiki waliwaokoa zaidi ya watu hamsini waliokuwa wanajaribu kuvuka na kuingia Italia kutoka Kaskazini mwa Afrika.Idadi hiyo ya wahamiaji ilitolewa baada ya habari kutolewa kuhusu maiti zilizopatikana.
Wanajeshi hao walisema kuwa watu waliofariki, walifariki kuokana na kukosa hewa kwani walikuwa katika sehemu ya chini ya mashua hiyo.
Mashua hiyo ilikuwa imewabeba takriban wahamiaji 600.
Mkasa wa huo unaonyesha hatari inayowakumba watu wanaotumia kila njia kufika barani ulaya ikiwemo kutumia vyombo ambavyo ni tishio kwa maisha yao.
Italia kwa mara nyengine imesema kuwa mataifa mengine ya ulaya hayafanyi lolote ili kulisaidia taifa hilo kuzuia maafa kama hayo.