Mgomo wa wafanyikazi wa Tazara wawahangaisha abiria
Sehemu kubwa ya wafanyakazi wa mamlaka ya reli ya Tanzania na Zambia TAZARA Stesheni ya Mbeya nchini Tanzania, wamegoma kufanya kazi tangu leo(jana) asubuhi.
Mgomo huo ambao wenyewe wameuita kuwa ni mgomo baridi umesababishwa na mamlaka hiyo kushindwa kuwalipa mishahara yao kwa miezi mitano sasa.Kwa majibu wa mwandishi wa BBC Baruan Muhuza ambaye yupo safarini kuelekea Kapiri Mposhi Zambia akitumia train ya TAZARA, mgomo huo umesababishwa kukwama kwa train hiyo kuendelea na safari yake hadi kufikia jioni hii.
MSIMAMO WAO
Amesema train ya abiria kutoka Dar es Salaam ilifika mjini Mbeya saa 4.30 asubuhi na hapo wafanyakazi hao waliipokea train hiyo kwa wimbo wa Solidarity forever.
Wafanyakazi hao wameiambia BBC kuwa wanailalamikia Serikali ya Tanzania kwa kuwapuuza madai yao huku serikali ya Zambia ikiwalipa wenzao wa upande wa pili.
Kwa muda mrefu TAZARA imekuwa katika kipindi kigumu cha uendeshaji wa shughuli zake kutokana na kukosa ruzuku ya serikali zote mbili.Baada ya mivutano na mikakati ya kuboresha shughuli za kabiashara ya mamlaka hiyo, iliamuliwa kuwa kila nchi iendeshe train yake na iishie mpakani kwenye miji midogo ya Tunduma (Tanzania) na Nakonde (Zambia).
TRENI KUISHIA MPAKANI
Mpango huo ndiyo kwanza umeanza kwa train ya abiria iliyoondoka jana Jumanne Dar es Salaam na nyingine ikitoka New Kapiri Mposhi na zitakutana mpakani baadae leo jioni.
Kwa mpango huo wasafiri wanaokwenda upande wa pili wa nchi nyingine watalazimika kushuka na kuingia kwenye train nyingine.
BBC inafuatilia kuona mchakato wa kuhamisha wasafiri hao utakavyokuwa, kwa kuzingatia miongoni mwa wanaosafiri kuna watoto, wazee vikongwe, wajawazito, Lakini pia kunakuwa na walemavu na wenye mizigo mingi.