Mtu akisoma tangazo kuhusu onyo dhidi ya maambukizo ya virusi vya ugonjwa wa Ebola mjini Monrovia, Liberia.
Mawaziri wa afya kutoka nchi za Afrika Magharibi wamekubaliana kuondoa upigaji marufuku wa safari za ndege na ufungaji wa mipaka kwa nchi ziliathirika kutokana na ugonjwa wa Ebola. Mawaziri hao ambao wamekutana mjini Accra, Ghana kupitia upya mikakati iliyokuwa ikitumika kupambana na virusi vya ebola pia wametoa ombi maalum kwa mashirika ya ndege kurejesha safari zao katika nchi zilizoathirika.
Mawaziri wa afya wamesisitiza mkakati wa pamoja kuwa bado ni mpango bora kabisa katika kupambana na ugonjwa wa ebola. Mawaziri hao wamezitaka nchi kutofunga mipaka yao kwa nchi zilizoathirika lakini wabakie kuwa waangalifu.Wamekubaliana kupeleka timu ya wataalam katika nchi hizo pamoja na kutoa misaada ya kibinadamu ambapo Ghana imekubali kuwa kituo cha kuratibu shughuli za misaada ya kibinadamu kwa nchi zilizoathirika katika eneo la Afrika Magharibi.Pia wamekubaliana kuongeza raslimali watu ikiwa ni pamoja kutakiwa haraka kwa wafanyakazi wa afya, vifaa vya kujikinga na ugonjwa huo, na vituo vya kuwahifadhi wagonjwa.
Shirika la Afya la Afrika Magharibi lina wiki moja ya kuandaa hatua za kuchukua na kuandaa bajeti ili kutekeleza mapendekezo yaliyotolewa kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani na wadau wengine.

Mawaziri wote wa afya isipokuwa wale wa kutoka nchi zilizoathirika kutokana na ugonjwa wa ebola za Guinea, Sierra Leone, Liberia na Nigeria walihudhuria mkutano huo.

Waliobaki hawakuweza kuhudhuria kutokana na matatizo ya ndani na matatizo ya usafiri wa ndege ambao umesitishwa katika nchi zilizoathirika.
Mawaziri wa faya wametoa ombi maalum kwa mashirika ya ndege kurejesha safari za ndege na kuendelea kuruka kwenda katika nchi zilizoathirika.
Hata hivyo wamesisitiza upimaji wa joto la mwili na kuhakikisha usafi wa mikono katika vituo vya kuingia na kutoka