Stori: Elvan Stambuli
MBUNGE wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangala amesema ametangaza nia ya kugombea urais ili aweze kupimwa na chama chake (CCM) na wananchi kama anafaa.

Akizungumza kwenye Ukumbi wa Hyatt Regencey Kilimanjaro Hotel jijini Dar es Salaam juzi, Dk. Kigwangala alisema ameamua kutangaza nia bila kutumwa na mtu au kikundi chochote isipokuwa amedhamiria kuongoza taifa.“Kipaumbele changu kitakuwa ni katika kuhakikisha madini, mito, bandari, reli, viwanja vya ndege, mazao vinanufaisha wananchi,” alisema.
Alisema kutokana na rasilimali zilizopo nchini, nchi yetu ilitakiwa iwe miongoni mwa nchi kumi tajiri katika Bara la Afrika. “Tuna kila kitu, madini ya Tanzanite, dhahabu, almasi, gesi, mito, maziwa, bandari na kadhalika, hakuna haja ya kuwa maskini,” alisema.Alisema akichaguliwa kugombea urais ataweka kipaumbele katika mambo yote yanayohusu  miundombinu  na utawala bora.
“Anatakiwa rais ambaye anachukia rushwa, ukwepaji wa kodi na alinde ardhi ya taifa,” alisema Kigwangala huku akisema yeye sifa hizo anazo na kinachotakiwa wananchi wampime.