Polisi Ufaransa wapiga doria usiku kucha.
Polisi nchini Ufaransa wameendelea na msako wa washukiwa wanaotuhumiwa kuwaua wafanyakazi wa gazeti la vibonzo la Charlie Hebdo.
Msako huo umeelekezwa zaidi katika jiji la Paris hasa katika mji wa Picardy,ulioko upande wa Kaskazini Mashariki mwa jiji la Paris.

Ulinzi umeimarishwa pia katika kijiji cha Longpont, ambapo msako unaendeshwa nyumba kwa nyumba ambao unaambatana na upekuzi.
Waziri wa mambo ya ndani wa Ufaransa Bernard Cazeneuve, ameeleza kuwa askari elfu themanini na nane wakiwemo maafisa wa ngazi za juu na askari wa kawaida wanashiriki katika msako huo na kwamba wametawanywa kila pembe ya jiji la Paris na vitongoji vyake tangu shambulio hilo litokee Jumatano.
Mapema jana wanaume wawili waliokuwa na silaha, wanaoaminika kuwa ni watuhumiwa wanaosakwa walivamia kituo kimoja cha mafuta, na kuna wasiwasi kwamba watuhumiwa hao wawili huenda wakarejea katika jiji hilo la Paris.
Ikiwa ni siku ya pili mfululizo maelfu ya wananchi wa jiji la Paris wamefanya ibada katika eneo la Place de la Republique kwa ajili ya kuwaombea watu kumi na wawili waliouawa kwenye shambulio la Charlie Hebdo. Taa za mnara wa Eiffel zilizimwa mwishoni mwa siku ya maombolezo. Mjini New York, wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa walisimama kwa muda kuwakumbuka waathrika wa shambulio hilo.
NB. Jana katika matangazo yetu ya Amka na BBC tuliwaarifu kwa makosa kwamba washukiwa katika lile shambulio dhidi ya jarida la Charlie Hebdo mjini Paris walikamatwa na polisi. Tunasikitika kwamba taarifa hiyo haikuwa sahihi kwa kuwa washukiwa hao wawili bado walikuwa wanasakwa.
Kwa niaba ya Amka na BBC, tunawaomba radhi wasikilizaji wetu wote kwa hitilafu hiyo ambayo haikukusudiwa.