kajalaKajala Masanja ‘Kay’
Dar es Salaam: Mtoto mzuri anayebamba kwenye Bongo Movies, Kajala Masanja ‘Kay’ amemuangukia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk John Pombe Magufuli ‘JPM’ kuwa kama ikitokea akatoa msamaha wa wafungwa, amkumbuke  mumewe, Faraji Agustino ambaye yupo gerezani Segerea jijini Dar akitumikia kifungo cha miaka saba.

Akizungumza na Amani hivi karibuni, Kajala alisema kuwa amekuwa akimuwaza mumewe huyo na suluhisho kuu kwa sasa litakalomfanya Faraji atoke gerezani ni msamaha wa rais pekee.
“Najua Mungu yupo na atatenda miujiza, namuomba sana Rais Magufuli siku akitoa msamaha kwa wafungwa amkumbuke na mume wangu Faraji,” alisema Kay.
Hata hivyo, mmoja wa wanasheria maarufu Dar aliliambia gazeti hili kuwa kosa alilopatikana nalo mume wa Kay huwa halina msamaha wa rais.
Machi 2013, Faraji alihukumiwa kifungo cha miaka saba jela au faini ya za zaidi ya Sh. milioni 200 baada ya kupatikana na hatia ya kutakatisha fedha haramu kwenye Benki ya NBC, Tawi la Dar ambapo jamaa huyo alishindwa kulipa kiasi hicho cha fedha na kujikuta ‘akiozea’ Segerea huku Wema Sepetu ‘Madam’ akimlipia Kajala faini ya Sh. Milioni 13, iliyomnusuru kwenda jela miaka mitano.