Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesisitiza msimamo wa serikali juu ya uamuzi wa kudhibiti uingizaji sukari holela, akisema lengo ni kulinda viwanda.
Hata hivyo amesema baada ya miaka minne, nchi itazalisha tani 420,000 ambazo ndiyo mahitaji ya sasa nchini ingawa uzalishaji ni tani 320,000.
Waziri Mkuu alisema hayo jana bungeni wakati akijibu maswali ya papo kwa papo ,baada Kiongozi wa upinzani bungeni,Freeman Mbowe kusema uhaba wa sukari nchini ulitokana na agizo la Rais John Magufuli kuzuia uingizaji sukari kutoka nje ya nchi bila kufuata utaratibu wa kisheria .

Mbowe alitaka kufahamu ikiwaserikali ilifanya uamuzi huo, ni nani aliagiza na iwapo uagizaji hautaathiri uzalishaji wa sukari nchini nakusababisha tatizo hilo kwa mwaka mzima?.
Akijibu swalihilo,Majaliwa alisema upungufu huo hauwezi kutatuliwa kwa kuingiza sukari nchini bila utaratibu na kudhibitiwa kwa kuwa inaweza kuingizwa sukari nyingi ikizingatiwa kwamba, ipo sukari ya aina mbili ya mezani na viwandani ambazo hazina tofauti kubwa kwa kuangalia.
Alisema ikishindikana kudhibitiwa, upo uwezekano wa kuletwa nchini sukari nyingi ya mezani na ikajaa sokoni.
“Kwa hiyo kauli ya rais ni kulinda viwanda vya ndani lakini jukumu la bodi sasa baada ya kauli ni kuratibu vizuri, kwa hiyo sukari imeratibiwa vizuri”alisema.
Alisema bodi ya sukari itaendelea na utafiti kujua ongezeko lawatu na mahitaji ili kufanikisha mahitaji ya soko.
Alisema Rais John Magufuli wakati wote anapotoa maagizo au matamko , yanatokana na mwelekeo na mpango wa serikali kwa lengo maalumu.
Majaliwa alisema ni kweli sukari inaratibiwa na bodi ya sukari kwa kuwa imewekwa kisheria kufanya utafiti na kusimamia viwanda vya ndani vinavyozalisha na kusambaza bidhaa hiyo itoshe.
Waziri mkuu alisema kwa miaka mitatu hadi minne iliyopita, sukari ilikuwa ikiletwa kwa utaratibu ambao waligundua unavuruga mwenendo wa viwanda vya ndani ambavyo havipati tija.
Alisema serikali ya awamu ya tano ilipoingia madarakani ikawa na mkakati wa kulinda viwanda vyandani kwa sukari inayoingia kudhibitiwa na kuhamasisha viwanda vya ndani kuzalisha zaidi.
Alisema mahitaji ya sukari nchini ni tani 420,000 huku uzalishaji ukiwa tani 320,000; hivyo kuwa na upungufu wa tani 100,000 .
Alisema ili mahitaji ya sukari ya tani 100,000 na inayotakiwa kuingizwa nchini isivuruge uzalishaji ujao, imefaywa na bodi ya sukari hivyo hata kuagiza na vibali vimefanywa na bodi yasukari.