TUME ya Maendeleo ya Ushirika inakusudia kuvifuta vyama 1,862 vya ushirika nchini, kutokana na kukiuka matakwa ya sheria ya vyama hivyo na kushindwa kutimiza masharti ya usajili wake.
Miongoni mwa vinavyofutwa ni Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo (Saccos) cha Madiwani wa Manispaa ya Kinondoni, Saccos ya Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), Madiwani Saccos ya Kagera na cha Madiwani wa Mpwapwa na vingine vya ushirika.

Akizungumza na wanahabari juu ya kusudio hilo, Kaimu Mrajisi wa vyama hivyo na Mtendaji Mkuu wa Tume hiyo, Dk Audax Rutabanzibwa alisema hatua watakazochukua baada ya kufuta vyama hivyo ni kuendelea kuwafuatilia waliosajili vyama hivyo na warajisi wasaidizi ili kubaini ukweli wa uanzishwaji wake.
Alisema kuna uwezekano waliosajili walishirikiana na warajisi wasaidizi ili kuanzisha vyama hewa kwa lengo la kujipatia fedha.
Alitaja vyama vitakavyofutwa kulingana na maeneo, kwa upande wa Arusha kuwa ni 83, Dar es Salaam 91, Dodoma 50, Geita 16, Iringa 74, Kagera 240, Katavi 19, Kigoma 38, Manyara 73, Mara 203, Morogoro 278, Mtwara 52, Njombe 18, Pwani 324, Rukwa 14, Ruvuma 14, Shinyanga 89, Simiyu 93, Singida 15, Tanga 77 na Lindi kimoja.
Aliongeza kuwa kutokana na sababu hizo, vyama vinavyokusudiwa kufutwa ni 1,862 na vitafutwa baada ya siku 90 kuanzia Mei 13, mwaka huu.