Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Bella Bird
BODI ya Wakurugenzi ya Benki ya Dunia imeidhinisha mkopo wa Dola za Marekani milioni 200 (zaidi ya Sh bilioni 400) kwa ajili ya usambazaji wa umeme vijijini nchini.
Taarifa iliyotolewa jana Dar es Salaam na Benki ya Dunia ilisema kuwa kuidhinishwa kwa mkopo huo, kutafanya jumla ya kaya milioni 2.5 za vijijini kuunganishwa kwenye umeme wa gridi ya taifa ndani ya miaka mitano ijayo.

Mpango huo una lengo la kuendelea mafanikio, ambayo yamefikiwa na nchi ya kuongeza watu wanaotumia umeme ambao kwa mwaka 2014 walifikia asilimia 36.
Taarifa hiyo pia iliongeza kuwa mpango huo, una lengo la kuhamasisha matumizi ya nishati jadidi maeneo ya vijijini pamoja na kuzijengea uwezo taasisi zinazozalisha umeme.
“Kupatiwa huduma ya umeme ni kupanua fursa za kiuchumi pamoja na kupunguza umaskini,” alisema Bella Bird ambaye ni Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania ambaye pia anawakilisha taasisi hiyo katika nchi za Malawi, Burundi na Somalia.