Mwanariadha mlemavu wa Afrika Kusini Oscar Pistorius, amefikishwa mahakamani bila ya miguu yake ya bandia, wakati wa kusikizwa na kuamuliwa kwa kesi ya mauwaji yanayomkabili.

Mwanariadha huyo alisimama kizimbani kwa mikongojo, akiinamisha kichwa chake, huku wakili wake Barry Roux, akirejelea kilichotukia usiku wa mauwaji ya mpenziwe Reeva Steenkamp, miaka mitatu iliyopita.
Alisema kuwa Bwana Pistorius, alipoteza kila kitu na hatoweza kurejea taaluma yake tena ya kukimbia.
Binamu wa Bi Steenkamp, Kim Martin, aliiambia mahakama hiyo kuwa mwanariadha huyo amekataa kuelezea namna mauwaji hayo yalivyotekelezwa.