Ziara ya Kikundi cha Wajasiriamali Wanawake kutoka Tanzania (Tanzania Saccos for Women Enterprenuers) imezaa matunda baada ya kikundi hicho cha kina mama kufanikiwa kuingia mkataba wa ushirikiano (MoU) katika masuala ya biashara na Kukundi cha Wanawake Wajasiriamali wa Comoro (Association of Women Entrepreneurs in Comoro).

Makubaliano hayo ya ushirikiano yalifikiwa kufuatia ziara ya siku mbili iliyofanywa na Kikundi cha Wajasiriamali Wanawake kutoka Tanzania nchini Komoro tarehe 14 Juni 2016. Lengo la ziara hiyo ilikuwa kutafuta masoko kwa ajili ya bidhaa za Tanzania nchini Komoro, pamoja na kukutana na wajasiriamali wa Komoro ili kuweza kubadilishana taarifa juu ya fursa mbalimbali za biashara kati ya Tanzania na Komoro.

Tukio hilo la utiaji saini wa makubaliano ya ushirikiano baina ya vikundi hivyo vya Wajasiriamali akina mama kutoka Tanzania na Komoro lilishuhudiwa na Balozi wa Tanzania nchini Komoro Mhe. Chabaka F. Kilumanga. Katika hafla hiyo, Mhe. Balozi Kilumanga aliwapongeza wajasiriamali hao kwa hatua hiyo muhimu waliofikia na kuwa ana imani ushirikiano huo utakuwa ni wakudumu na wenye manufaa kwa pande zote mbili. Alieleza kuwa Tanzania na Komoro zinaweza kushirikiana katika nyanja mbalimbali za biashara na ana imani kuwa hii itakuwa ni chachu kwa wawekezaji wengine kutoka Tanzania kuja nchini Komoro kwa ajili ya kuekeza.
Bi. Naila Thabeet wa Association of Women Enterpreneurs akibadilishana mkataba na Bi. Anna Matinde kutoka Tanzania Saccoss for Women Enterprenuers.
Wadua wakishuhudia tukio la kihistoria ambapo ni mara ya kwanza vikundi vya akina mama kutoka Komoro na Tanzania wamekubaliana kushirikiana katika nyanja za biashara.