Kati ya wanafunzi 393,734 waliokalia mtihani wa kidato cha nne nchini Tanzania mwaka uliopita,takriban wanafunzi 24,528 ambao walipita mtihani huo huenda wasijiunge na kidato cha tano mara moja kutokana na uhaba wa madarasa.

Kulingana na gazeti la The Citizen nchini humo wale watakaoathiriwa ,ni pamoja na wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na taasisi za kiufundi zilizopo nchini humo.
Shule za uma hazitaweza kuchukua wanafunzi wote waliofuzu kuendelea na kidato cha tano.
Akitangaza matokeo hayo ya wanafunzi waliochaguliwa ,waziri katika ofisi ya rais anayesimamia utawala wa kijimbo na serikali za mtaa Bw George Simbachawene alisema: ''ni swala lenye changamoto lakini tunafanya juhudi kuhakikisha kuwa madarasa zaidi yanajengwa ili wanafunzi wote waliofuzu waendelee na masomo''.
Kulingana na The Citizen,amesema kuwa wanafunzi walioachwa nje ni pamoja na wasichana 6,789 na wavulana 17,739.