Waziri wa Fedha, Dk Philip Mpango akiwasilisha bajeti ya serikali ya mwaka 2016/17 bungeni hivi karibuni.
WASOMI nchini na wadau mbalimbali wameunga mkono Bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/17. Pia, wameunga mkono hatua ya serikali ya kuanzisha mfumo wa kuwakata kodi wabunge katika malipo yao ya kiinua mgongo baada ya kutumikia ubunge kwa miaka mitano.
Wamesema kama wabunge wataonekana wakati wa kuijadili bajeti hiyo, wakipinga suala la kulipa kodi katika kiinua mgongo chao wanacholipwa baada ya miaka mitano, watakuwa wabinafsi na siyo raia wema.

Walisema hayo walipokuwa wakitoa maoni yao kuhusu Hotuba ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/2017, iliyowasilishwa bungeni mjini Dodoma juzi na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango (pichani).
Walieleza kuwa maamuzi ya kuwataka wabunge kulipa kodi hiyo yamechelewa, kwani kwa miaka kadhaa wamekuwa hawalipi kimakosa, kwani wanalipwa fedha nyingi huku wananchi wanaopata mishahara midogo wakilipa kodi.
Walieleza bayana kuwa ulipaji kodi unawahusu watu wote kuanzia rais hadi mkulima hivyo wabunge walikuwa wakikosesha mapato halali ya serikali. Ngowi, Bashiru, Bana walonga Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Profesa Honest Ngowi alisema suala la wabunge kulipa kodi limechelewa, kwani wengine wote wanalipa kodi na wao hawawezi kuwa juu ya wengine.
Alisema kwa kuwa ni pendekezo la serikali na wabunge ambao ndiyo wanatakiwa kupitisha, watajadili kutokana na kuwahusu kutakuwa na mgongano wa kimaslahi, lakini iwapo watakataa watakuwa wabinafsi sana.
Naye Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Bashiru Ally alisema kodi inakusanywa kwa lengo la kunufaisha watu wote kuanzia ngazi ya rais hadi mkulima kulingana na vipato vyao, hivyo hakuna mgogoro kwa wabunge nao kulipa kodi kwa mapato yao.
Dk Ally alisema anatarajia wabunge wataelewa na kuona ni haki yao kulipana, ikiwa watajadiliana na kujenga hoja kwa lengo la kupata msamaha wa kodi kama ilivyokuwa awali itaangaliwa hoja husika.
“Nasema ni msamaha kwani siyo haki yao kutolipa kodi ni lazima kulikuwa na sababu na kama kuna mantiki kodi itaondolewa lakini kwa hoja yenye mantiki vinginevyo hawana sababu ya kutokulipa kodi,” alieleza Dk Ally.
Mhadhiri mwingine wa UDSM, Dk Benson Bana akieleza kuwa suala la wabunge kulipa kodi, licha ya kuwa limechelewa kutekelezwa, lakini kwa mwaka 2020 wamewapa taarifa mapema.
Dk Bana alisema wabunge wamekuwa wakilipwa fedha nyingi, lakini hawalipi kodi jambo ambalo walikuwa si raia wema kwani raia mwema anatakiwa kulipa kodi kwa kile anachopokea.
“Ikiwa katika kujadili hotuba watatokea wa kupinga wataaibika kwani hawatakuwa na sifa ya raia mwema ya kuunga mkono jitihada za serikali kulipa kodi na watashangaza kwa kukwepa wajibu wao kwa kutotenda haki,” alifafanua Dk Bana.
Waziri Mkuu IMTU aunga mkono Naye Waziri Mkuu wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Tiba na Afya cha IMTU cha jijini Dar es Salaam, Adili Msika alisema jana kuwa moja ya maeneo yaliyopongezwa na wananchi wengi hususani wanafunzi ni hatua ya kuanza kukatwa kodi kwa kiinua mgongo cha wabunge.
Msika alisema inashangaza kuona kuwa wakati wabunge wamekuwa wakionesha kukerwa na wingi wa misamaha ya kodi na mianya ya kukwepa mapato na kupunguza mapato ya serikali, lakini nao wamekuwa katika kundi la watu wanaoshindwa kutimiza wajibu wa kulipa kodi halali za serikali.
“Wabunge kama wawakilishi wa wananchi na watunga sheria wanapaswa kuwa mfano. Haiingia akilini kuona wabunge wanashiriki kutunga sheria za kuwatoza kodi wananchi masikini wanaofanya kazi serikalini au wanaofanya biashara ndogo ndogo huku wenyewe wakipewa kiinua mgongo bila kukatwa kodi,” alisema Msika.
Alisema kutokana na ukubwa wa fedha za kiinua mgongo, ambazo wabunge wamekuwa wakilipwa baada ya kukoma kwa kipindi chao cha ubunge cha miaka mitano, serikali imekuwa inapoteza kiasi kikubwa cha mapato na kusema wakati umefika kwa serikali kuanza kukusanya fedha hizo.
Katibu Mkuu mstaafu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE), Ally Kiwenge, akizungumzia hatua hiyo ya kuanza kukatwa kodi kwa fedha za kiinua mgongo cha wabunge, alisema mpango huo lazima uungwe mkono kwa sababu unatengeneza usawa.
“Hii ni hatua ya kuungwa mkono na kila Mtanzania. Nafahamu wabunge watacharuka na kushinikiza mpango huo ufutwe, lakini wananchi na wanaharakati ni lazima wasimame imara kuhakikisha kuwa hilo linatekelezeka ili kuleta usawa,” alisema Kiwenge.
Kodi ya Majengo, Mahakama ya Mafisadi Aidha, Profesa Ngowi alizungumzia ukusanyaji wa kodi ya majengo kufanywa na Mamlaka ya Mapato (TRA) kuwa kama wameboresha mapungufu ya zamani, yaliyofanya kodi kupelekwa katika halmashuri na kuwepo na utaalamu wa makadirio, basi suala hilo litakuwa sahihi, lakini kama hakuna maboresho hakutakuwa na jipya.
Aliitaka serikali na wabunge katika majadiliano, kuangalia suala la utozaji kodi kwa sekta ya utalii ya asilimia 18, kwani Kenya ambayo ni mshindani mkubwa wa sekta ya utalii inatoza asilimia 16 hivyo isije kuathiri mapato.
Akizungumzia kutengwa fedha kwa ajili ya Mahakama ya Mafisadi, Dk Ally alitaka iwe kwa muda na dharura kwa kuwa hali ya sasa ni mbaya, lakini isiwepo mahakama kama ni kosa la kudumu, bali nchi iwekeze katika mifumo imara ya uwajibikaji ili mafisadi wasipatikane.
Alisema kwa mifumo hiyo, itafanya nchi kuwa kama enzi za Mwalimu Julius Nyerere ambako hakukuwa na watu wa kujilimbikizia mali, kwani mafisadi ni watu wenye madaraka makubwa siyo watendaji wa kata ambao wanaathiri maendeleo ya nchi.
Naye Dk Bana aliongeza kuwa licha ya kuwa bajeti ni nzuri, lakini serikali ilitakiwa kuangalia vyanzo vipya vya mapato bila kutengeneza bajeti yenye kumfikiria zaidi mwananchi wa mjini badala ya yule wa vijijini na maeneo ya pembezoni.
Alisema ulipaji kodi ya majengo ni ya kikoloni ingeondolewa bila kuathiri mapato kwa kutoza ya biashara pekee na siyo makazi kwani kuna wastaafu wamejenga nyumba zao lakini wanakabiliwa na ulipaji kodi ambayo hawana.
“Wakati serikali inahamasisha kuwa na nyumba bora lakini bado wanatoza faini hivyo kurudisha nyuma jitihada za serikali ni vyema hili la nyumba za kuishi kuangaliwa kwani ni usumbufu sana,” alieleza.
VAT za benki, simu yatia doa Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Fedha ya Dhow, Profesa Mohamed Warsame alisema pamoja na nia njema ya serikali ya kuboresha maisha ya wananchi masikini, lakini hatua ya kuanzisha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye huduma za kibenki na tozo kwenye huduma ya kutuma fedha kupitia simu za mkononi, kunaweza kukuza gharama kwa wananchi.
Alisema katika kipindi hiki ambacho wananchi wanapaswa kupata huduma za kibenki ikiwemo mikopo kwa urahisi na bila masharti magumu, hatua ya serikali ya kuanzisha VAT kwenye mambo hayo mawili kunaweza kufanya wamiliki wa benki kutumia nafasi hiyo kuwaumiza wananchi.
“Ni lazima serikali iliangalie hili suala kwa mapana yake. Ni vyema mpango huu ukaenda sambamba na kuanzishwa kwa sera za udhibiti kwa benki kutumia kisingizio hicho kupaisha gharama za benki na pia kampuni za simu kutumia mwanya huo kuwaibia wananchi na kujinufaisha,” alisema Profesa Warsame.
Aidha, alisema ni lazima pia serikali iwe makini na hatua ya kuanza kutoza kodi ya asilimia 10 katika bidhaa za karatasi kwa vile hatua hiyo inaweza kutia doa nia njema ya serikali ya kukuza kiwango cha elimu nchini pamoja na sera yake nzuri ya kutoa elimu bure kuanzia darasa la saba hadi kidato cha nne.
“Nasema hivi kwa vile wafanyabiashara hasa wale wanaochapisha vitabu vya elimu au vijarida mbalimbali na hata wachapishaji wa magazeti wanaweza kutumia mwanya huo kupandisha bei za uchapaji na kuongeza mzigo kwa wananchi katika kupata vitabu na vijarida vya kielimu,” alisema.
CCM yataka vitendo Naye Msemaji wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Christopher ole Sendeka amesema Watanzania watayafikia maendeleo yanayokusudiwa katika mwaka mpya wa fedha, ikiwa watashiriki kuitekeleza bajeti mpya kwa vitendo.
Kwa mujibu wa Ole Sendeka, bajeti hiyo imekuja na majibu ya kero karibu zote za Watanzania hivyo ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha inafanikiwa kwa kutoa ushirikiano unaostahili kupitia uwajibikaji katika maeneo ya kazi, iwe kwenye sekta binafsi au serikalini.
“Bajeti ni nzuri na Watanzania hawana budi kukubali na kuelewa kuwa wakati wote nchi inapoamua kuingia katika mabadiliko chanya ya kiuchumi, haiwezi kufanya hivyo na kufanikiwa kwa mara moja, bali kwa hatua inayohitaji ushiriki wa kila mmoja hasa katika uzalishaji.
“…Kwa maana hiyo, tunapaswa kuipa nafasi serikali huku tukiisaidia kuhakikisha matumizi mazuri ya fedha za umma, pamoja na uwajibikaji katika uzalishaji na kulipa kodi zote zinazostahili kulipwa,” alisema.
“Hatua ya kufikia kuona kuwa taasisi za dini zinapaswa kulipa kodi kwa bidhaa zinazoziingiza nchini italeta usawa miongoni mwa walipa kodi kwa sababu wengi walikuwa wakizitumia kuingiza bidhaa zao kwa kupitia msamaha wa kodi uliokuwepo, zipo taasisi za dini zinazojiendesha kibiashara kupitia huduma za vyuo vikuu na nyinginezo, hizi zinastahili kulipa kodi,” alisema.
Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha DP, Abdul Mluye alisema ushiriki wa wananchi kuitekeleza kwa vitendo ndio utakaowezesha kuifanikisha. Mjadala kuhusu bajeti hiyo utafanyika kwa siku saba kuanzia leo bungeni baada ya wabunge kutumia siku ya jana kusoma na kutafakari hotuba ya Dk Mpango yenye thamani ya Sh trilioni 29.5.
Imeandikwa na Oscar Mbuza na Theopista Nsanzugwanko, Dar na Namsembaeli Mduma, Dodoma.