Rais Dk John Magufuli.
UAMUZI wa Serikali wa kuwakata kodi kwenye kiinua mgongo chao viongozi wa kisiasa akiwemo Rais John Magufuli, umepongezwa na wasomi na wanasiasa, wakieleza unaleta usawa katika jamii.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana na gazeti hili, wasomi hao walisema ilikuwa ni mazoea mabaya kuwaacha viongozi wanasiasa kutolipa kodi wakati wanapomaliza muda wao; wakati watumishi wa kawaida ambao vipato vyao ni vidogo walikuwa wanakatwa kodi kwenye kiinua mgongo chao.

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Profesa Honest Ngowi, alisema uamuzi huo umeifanya serikali kuwa na chanzo kipya cha mapato, lakini pia ni uamuzi ambao umeleta haki katika jamii. “Maamuzi haya yalitakiwa kufanywa miaka ya nyuma, niseme tumechelewa sana maana hawa viongozi wanahudumiwa kila kitu na kupatiwa matibabu, ki ukweli wana maisha mazuri. Kitendo cha kuwasamehe kodi kwenye kiinua mgongo chao haikuwa halali,” alisema Profesa Ngowi.
Alisema hatua hiyo ilikuwa inaongeza pengo la kipato kati ya wananchi wa kawaida na viongozi wa kisiasa, kwani ilikuwa viongozi ambao wana maisha mazuri wanaongezewa faida nyingine ya kutokatwa kodi na mtumishi wa kawaida, ambaye anapata mshahara mdogo alikuwa analipa kodi anapostaafu. Hata hivyo alisema matunda ya uamuzi huo wa serikali, yataanza kupatikana baada ya miaka mitano.
“Hivyo hakuna fedha itakayoingia mwaka ujao wa fedha hadi mwaka 2020 ndipo serikali itapata kodi hiyo kutoka kwa viongozi wanasiasa wastaafu,” alisema. Wasomi kwenye siasa Alisema uamuzi huo wa serikali, pia unaweza kusaidia kupunguza kasi ya wasomi kuingia kwenye siasa maana watafahamu kwamba kuanzia sasa baadhi ya vivutio vilivyokuwepo vinaanza kuondolewa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kupunguza Umasikini (Repoa), Dk Donald Mmari alisema uamuzi wa viongozi wa kisiasa, kukatwa kodi kwenye kiinua mgongo chao ni jambo jema kwa sababu ni kada, ambayo kiinua mgongo chao ni kikubwa na kutokatwa kodi haki haikuwa inatendeka.
Alisema watumishi wa umma wanapata kiinua mgongo kidogo, kutokana na mishahara yao kuwa kidogo, lakini wamekuwa wanakatwa kodi, hivyo wanasiasa nao kukatwa kodi huo ndio kanuni ya usawa katika ulipaji wa kodi. “Huduma zote tunapata sawa, barabara tunatumia wote, hivyo kanuni ya kodi ni kwamba anayepata zaidi alipe zaidi, kitendo cha kutolipa kodi kilitokana na wanasiasa kujipendelea tu,” alisema Dk Mmari.
Aliongeza kuwa kisingizio kwamba wanasiasa hawana pensheni kama watumishi wengine wa umma, sio jambo la kutilia maanani, kwani watumishi wa umma ambao wanafanya kazi kwa mikataba wanapomaliza mikataba yao wanalipwa kiinua mgongo ambacho pia kinakatwa kodi.
Alisema kama wabunge na wanasiasa wengine walioko madarakani, wana fursa ya kupata mikopo ya kununua magari, kuna watumishi wa umma ambao hawana fursa hiyo na hao ndio ambao wamekuwa wanalipa kodi kwa Serikali.
Profesa Haji Semboja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema kilichofanywa na Serikali kuwakata kodi wanasiasa kwenye kiinua mgongo chao, sio jambo baya kwani sababu za awali zilizokuwa zinafanya wasikatwe au kusamehewa kodi kwa sasa hazipo tena.
Alisema miaka ya nyuma, wanasiasa waliondolewa kodi kwenye viinua mgongo vyao kwa kuamini kuwa wakimaliza kazi zao za siasa, hawawezi kupata kazi tena na ilikuwa ni moja ya kuvutia watu wasomi waingie kwenye siasa isaidie kupata viongozi wa kisiasa. “Lakini kwa sasa wasomi ni wengi na siasa imekuwa kazi kama ilivyo kazi zingine, leo hii mtu akiacha siasa anaenda kufanya kazi nyingine.
Mfano Mzee Pinda (Mizengo Waziri mkuu mstaafu) kwani hana income (kipato) nyingine? Jibu ni kwamba anayo,” alisema Profesa Semboja. Aliongeza kuwa ni mazoea mabaya kwa watu ambao wanapata kipato kikubwa, kutokatwa kodi huku anayepata kipato kidogo ndiye akatwe kodi. Alisema wakati umefika sasa wa kuachana na mazoea hayo mabaya na kwamba sababu za kusamehe wanasiasa wasikatwe kodi hazipo tena.
Alisema kilichofanywa na Serikali ya Rais John Magufuli sio jambo baya kwani siasa ni sawa na kazi nyingine na mwanasiasa muda wake ukiisha anafanya kazi nyingine. Usawa kwa watumishi Mwanaharakati wa Haki za Binadamu, Onesmo Olengurumwa, alisema kilichofanywa na Serikali ni jambo jema kwa maelezo kuwa wanasiasa ni watumishi kama ilivyo watumishi wengine na hivyo uamuzi wa Serikali ni wa kuleta usawa miongoni mwa watumishi wote.
Olengurumwa alisema iwapo wabunge na mawaziri, watakatwa kodi watakuwa makini kusimamia kodi hizo, zilete maendeleo na kwamba zitasaidia pia na wanasiasa hao, kuendelea kupata mishahara yao. “Hivyo mimi naona hiki kilichofanywa na Serikali ni kuleta usawa, wanasiasa walipewa upendeleo sana na hata kutungiwa sheria ya kulinda maslahi yao, sasa kama hili limeondolewa ni haki imetendeka kwa watu wote,” alisema Olengurumwa.
Alihadharisha kuwa kodi hiyo ya wastaafu haiwezi kuleta tija kwenye uchumi wa nchi kwa kuwa kitakachofanyika hapo ni kama serikali imepunguziwa mzigo wa kulipa wanasiasa wastaafu. “Hapo kama mbunge alitakiwa kulipwa Sh milioni 200 atalipwa Sh 180 kwa hiyo fedha zinazozunguka ni zile zile, kuna haja ya serikali kuangalia kupanua wigo kutoka kwenye mapato yanayotokana na rasilimali za nchi yetu,” alisema mwanaharakati huyo.
Alisema kuna nchi hazina rasilimali nyingi kama ilivyo kwa Tanzania, lakini wananchi wake wamekuwa wanafaidika na mapato ya rasilimali hizo kidogo, hivyo akashauri kwamba umefika wakati wataalamu serikalini wakune vichwa kuona namna serikali inavyoweza kupata mapato mengi kutokana na hizo rasilimali.
Ma DC waridhika Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Yahaya Nawanda, alisema suala la viongozi wa kisiasa kukatwa kodi kwenye kiinua mgongo chao amelipokea kwa furaha kwa sababu mtumishi yeyote wa umma anatakiwa kulipa kodi. “Naipongeza Serikali yangu kwa kuanzisha jambo hili, maana kulipa kodi ni jambo jema kwani inalenga kuboresha maisha ya Mtanzania,” alisema Nawanda.
Alisema bila kulipa kodi nchi haiwezi kupata maendeleo na hivyo yeye binafsi anaunga mkono uamuzi huo ili kupeleka mbele maendeleo ya wananchi. “Bila kodi hakuna mishahara hii tunayolipwa na hakuna nchi iliyoendelea bila wananchi wake kulipa kodi, hivyo wanasiasa kukatwa kodi kwenye kiinua mgongo ni jambo jema.”
Nawanda alisema wanasiasa ambao ni viongozi wa wananchi, wanatakiwa walipe kodi, wawe mfano kwa wananchi na kuwajengea tabia wananchi kulipa kodi bila shuruti. Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Humphrey Polepole alisema uamuzi wa viongozi wa kisiasa, kukatwa kodi kwenye kiinua mgongo chao tayari umepitishwa na Bunge na hivyo watu wanatakiwa kuutekeleza na kuusimamia.
“Kwa taratibu za nchi yetu tulizojiwekea, Bunge ndilo linapitisha Bajeti na kutunga sheria, jambo hili ambalo umeniuliza tayari limepitishwa na Bunge, hivyo sisi tunatakiwa kutii na kuheshimu uamuzi huo, kitendo chochote cha kuchallenge (kuhoji) uamuzi huo ni ukiukwaji wa taratibu za nchi,” alisema Polepole.
Juzi Bunge limepitisha Bajeti ya Serikali huku miongoni mwa marekebisho yaliyofanyika ni kwa viongozi wa kisiasa akiwemo Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Wabunge kukatwa kodi kwenye kiinua mgongo chao.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango aliliambia Bunge kwamba Rais Magufuli amekubali yeye kiinua mgongo chake pamoja na viongozi wengine nacho kikatwe kodi. Hatua hiyo ya Rais Magufuli ilikuwa ni majibu kwa wabunge, ambao walikuwa wanalalamika kwamba kwa nini viongozi wengine wa kisiasa wameachwa katika mpango huo.