Mtu mmoja aliyekuwa na Kisu na Shoka amewashambulia abiria waliokuwa kwenye Treni Kusini mwa Ujerumani usiku wa jumatatu na kuwajeruhi watu wanne kabla yeye kupigwa risasi na Polisi na kufa alipokuwa akikimbia baada ya tukio hilo.
Polisi wa mjini Wuerzburg wameeleza kwenye ukurasa wao wa Facebook kuwa abiria watatu wamejeruhiwa vibaya na wengine 14 wanapata msaada wa kitabibu kutokana mshtuko walioupata.

Polisi wamesema bado hakuna taarifa yeyote kuhusu sababu ya kutekelezwa kwa shambulio hilo.
vyombo vya habari vya Ujerumani vimemnukuu msemaji wa wizara ya mambo ya ndani mjini Bavaria kuwa mtu huyo ni mvulana wa miaka 17, mkimbizi mwenye asili ya Afghanistan.
Mwaka jana Ujerumani iliwaandikisha wahamiaji milioni moja waliokuwa wakiingia nchini humo, zaidi ya 150,000 raia wa Afghanistan.
Tangu mashambulizi ya hivi karibuni ya wanamgambo wa kiislamu nchini Ufaransa, kumekuwa na hali ya hofu ya kutokea mashambulizi kama hayo nchini Ujerumani, lakini mpaka sasa hakuna ishara zozote kuwa shambulio hilo lilikua la kigaidi.