Utafiti mpya umeonesha kwamba wanaume wa Uholanzi ndio warefu zaidi duniani, na upande wa wanawake, wanawake wa Latvia ndio warefu zaidi.
Kimo cha wastani kwa wanaume Uholanzi ni futi 6 kwa sasa (sentimeta 183), na kimo cha wastani kwa wanawake wa Latvia ni futi 5 inchi 7 (sentimeta 170).
Utafiti huo, ambao matokeo yake yamechapishwa kwenye jarida la eLife, umefuatilia kimo cha watu na mabadiliko yaliyotokea katika mataifa 187 tangu 1914.
Utafiti huo umebaini kwamba wanaume wa Iran na wanawake wa Korea Kusini ndio walioongeza kimo zaidi, wakiongeza kimo cha wastani kwa zaidi ya inchi 6 (sentimeta 16) na inchi 8 (sentimeta 20) mtawalia.
Wanawake wafupi zaidi duniani wanapatikana nchini Guatemala huku wanaume wafupi wakitokea Timor Mashariki.

UholanziImage copyrightEPA
Image captionMaafisa wa polisi nchini Uholanzi

Mwanamke wa umri wa miaka 18 kwa wastani nchini Guatemala alikuwa na kimo cha futi 4 inchi 7 (sentimeta 140) mwaka 1914 utafiti wa kwanza ulipofanywa na sasa kiwango hicho hakijafika kabisa futi 4 inchi 11 (sentimeta 150).
Kimo cha wastani kwa wanaume Timor Mashariki ni futi 5 inchi 3 (sentimeta 160).
Watafiti hao wanasema kuwa chembe chembe za jeni hubadilikabadilika, lakini cha muhimu zaidi ni kuwepo kwa lishe bora, usafi na matibabu ya hali ya juu.

Mataifa yenye wanaume warefu zaidi duniani 2014 (kwenye mabano ni nafasi iliyoshikiliwa 1914):

  1. Uholanzi (12)
  2. Ubelgiji (33)
  3. Estonia (4)
  4. Latvia (13)
  5. Denmark (9)
  6. Bosnia na Herzegovina (19)
  7. Croatia (22)
  8. Serbia (30)
  9. Iceland (6)
  10. Jamhuri ya Czech (24)

Mataifa yenye wanawake warefu zaidi duniani 2014 (kwenye mabano ni nafasi iliyoshikiliwa 1914):

  1. Latvia (28)
  2. Uholanzi (38)
  3. Estonia (16)
  4. Jamhuri ya Czech (69)
  5. Serbia (93)
  6. Slovakia (26)
  7. Denmark (11)
  8. Lithuania (41)
  9. Belarus (42)
  10. Ukraine (43)