Waziri Mkuu wa Uturuki, Binali Yildirim, ameelezea jaribio la mapinduzi la jana usiku, kuwa doa jeusi katika demokrasi ya Uturuki.
Na kaimu mkuu wa jeshi la Uturuki, ametangaza kwenye televisheni, kwamba jaribio la mapinduzi limeshindwa. Jenerali Umit Dundar alisema, wapanga njama 104 wameuwawa.

Lakini imetangazwa kuwa watu wengine 161 polisi na raia, kama ilivyosemwa, wamekufa wakipigania uhuru wa nchi yao.
Usiku kucha, miji ya Ankara na Istanbul ilivuma milio ya risasi na milipuko. Wakuu wanasema wanajeshi zaidi ya elfu 1500 wamekamatwa.
Waziri wa Uturuki anayeshughulika na Umoja wa Ulaya, Omer Celik, amesema hali sasa imerejea kuwa kawaida kwa asilimia 90, lakini baadhi ya makamanda bado wanazuwiliwa kama mateka.