Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri akipokea madawati 350 yenye thamani ya shilingi milioni 58 kwa shule 12 za msingi katika wilaya ya Tabora, kutoka kwa Mkurugenzi wa Tigo Kanda ya Ziwa Ally Maswanya(kulia), makabidhiano hayo yaliofanyika shule ya Msingi Mihayo iliyopo manispaa ya Tabora jana.


Mkurugenzi wa Tigo Kanda ya Ziwa Ally Maswanya Akisalimiana na wanafunzi wa  shule ya msingi Mihayo mara baada ya   makabidhiano hayo yaliofanyika shuleni  hapo  iliyopo manispaa ya Tabora jana.

Wanafunzi wa  shule  ya msingi Mihayo waakifurahia madawati mara baada ya makabidhiano hapo shuleni

Julai 18 2016 Tabora: Kampuni ya Tigo Tanzania imetoa msaada wa madawati 350 yenye thamani ya shilingi milioni 58 kwa shule 12 za msingi katika wilaya ya Tabora(50),Nzega(200) na Urambo(100) ikiwa ni mchango wa kampuni hiyo katika kuisaidia serikali kukabiliana na upungufu wa madawati katika shule za msingi nchini.



Akizungumza leo katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika katika shule ya msingi Mwangoye katika manispaa ya Tabora, Mkurugenzi wa Tigo Kanda ya Ziwa Ally Maswanya amesema mchango huo ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya kampuni hiyo ya kuunga mkono jitihada mbalimbali za kuleta maendeleo nchini.


“Mchango huu ni sehemu ya jitihada mbalimbali zinazofanywa na Tigo katika kusaidia utekelezaji wa miradi yenye tija kubwa kwa jamii. Tunaamini kwamba kupitia msaada huu, Tigo inatoa mchango wake katika kujenga viongozi wa baadaye wa taifa hili na wanataluuma mbalimbali wakiwamo madaktari, wahandisi na wengineo, "amesema Maswanya.

Maswanya amesema mwaka jana Tigo ilikabidhi msaada kama huo wa madawati katika shule za msingi katika mikoa ya Shinyanga, Mbeya, Iringa, Morogoro, Dar es Salaam, Mwanga  na kuongeza kwamba kampuni hiyo itaendelea kutoa madawati zaidi sehemu mbalimbali nchini siku za zijazo.

Makabidhiano yalihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa wa Tabora mheshimiwa Aggrey Mwanri ambaye alisema madawati hayo 350 yataboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto katika Mkoa wa Tabora na kutoa wito kwa wadau wengine kuunga mkono zoezi hilo.
“Tunapenda kutoa shukrani zetu za dhati kwa kampuni ya Tigo kwa kuwa mdau muhimu kwetu katika jitihada zinazoendelea za kujaribu kupunguza tatizo la ukosefu wa madawati ya kutosha katika shule za msingi za mkoa wetu wa Tabora. Ni dhahiri kwamba msaada huu wa madawati 350 yatawawezesha mamia ya wanafunzi wetu kupata sehemu za kukaa na hivyo kujipatia elimu zao katika mazingira bora zaidi,” alisema Mwanri.

Madawati hayo 350 yametolewa Tabora kwa shule za msingi 12 kama ifuatavo, Mihayo,Kasela,Shigamba,Itobo,Mwamala,Mwangoye,Umoja,Urambo,Ukombozi,Ussoke, Tulieni na Mabatini.