Mwenyekiti
wa Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA Mh.Freeman Mbowe,
amesitisha shughuli za maandamano zilizokuwa zimepewa jina la (UKUTA)
kwa Muda wa mwezi mmoja,kwa kile alichodai baada
ya kuombwa na viongozi wa Dini na taasisi Mbalimbali, ambapo maandamano
hayo yalitarajiwa kufanyika kesho Septemba Mosi nchi nzima.

Viongozi mbalimbali wa kidini pamoja na Taasisi mbalimbali za kiraia hatimaye wamesaidia kutokomeza UKUTA kwa kuuomba uongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kuahirisha Oparesheni hiyo iliyopangwa kufanyika Septemba mosi nchi nzima. 

Akizungumza na Waandishi wa Habari katika Makao Makuu ya CHADEMA Mwenyekiti wa Chama hicho Taifa,  Freeman Mbowe amesema  Viongozi hao wakuu wa kidini wamewaomba na kuwasihi katika vikao mbalimbali walivyokaa pamoja nao na kusema tunaheshimu viongozi hao. 

Mbowe amesema wanawapa muda wa wiki mbili au tatu ili waonane na Rais Magufuli kwa lengo la kutafuta suluhu ya kudumu ya mgogoro huu wa kisiasa na kuliepusha taifa na machafuko ya kisiasa. 

Pia amesema Viongozi wa Taasisi za kiraia kama vile Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu LHRC, Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Jukwaa la Wahariri na Jukwaa la Katiba nao wamewasihi kuahirisha UKUTA kwa muda ili kutoa fursa kwa jitihada za mazungumzo na majadiliano kufanyika. 

"Sisi CHADEMA tunatambua na kujali haki zetu za kisiasa kama zilivyofafanuliwa katika Katiba na Sheria za nchi yetu. Hata hivyo tunajali na kuheshimu kwa kiasi kikubwa zaidi haki za Watanzania ya kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yao" amesema Mbowe

Amesema wanawaomba kuwatangazia viongozi weo wa ngazi zote CHADEMA, pamoja na wanchama,wafuasi na Watanzania wote kuhairisha kwa mwezi mmoja mikutano na maandamano ya amani yaliyopangwa kufanyika nchi nzima kuanzia kesho Septemba Mosi.