Serikali ya Tanzania imezisimamisha kwa muda stesheni mbili za redio ,radio 5 na Magic FM kwa madai ya kumtusi rais Magufuli na kuchochea ghasia nchini.
Mapema mwezi huu ,serikali pia ilipiga marufuku gazeti moja kwa kuchapisha 'habari za uongo'.

Waziri wa mawasiliano Nape Nnauye amesema ameagiza kamati ya maadili kuzichunguza idhaa hizo na kupendekeza hatua zaidi kuchukuliwa dhidi yake.
Marufuku ya steheni hizo mbili inajiri huku hali ya wasiwasi ikitanda nchini humo kufuatia hatua ya upinzani kufanya mikutano yake nchi nzima.
Kulingana na muungano wa upinzani nchini humo CHADEMA,mikutano hiyo kwa jina UKUTA ,inalenga kupinga kuidhinishwa kwa sheria ya uhalifu wa mitandaoni inayokandamiza uhuru wa kujieleza ,kufutwa kazi kwa wafanyikazi wa serikali kiholela pamoja na marufuku ya mikutano ya kisiasa ya upinzani.
Ubalozi wa Marekani mjini Dar es Salaam umetoa ushauri wa kusafiri kwa raia wake ukiwaonya kutozuru maeneo ambayo mikutano hiyo itafanyika.