Mmoja wa waigizaji nyota wa filamu za televisheni nchini Brazil, Domingos Montagner, amefariki akiigiza moja ya filamu mashuhuri sana za televisheni, ambazo hufahamika kama 'soap operas', nchini humo.
Montagner alikufa maji mtoni eneo ambalo yeye na wahusika wengine walikuwa wakirekodi kisa kimoja cha filamu hiyo.
Montagner aliigiza kama mhusika mkuu katika filamu hiyo ya Velho Chico, iliyopewa jina la mto huo wa Sao Francisco katika jimbo la Sergipe, kaskazini mashariki mwa nchini hiyo, ambapo alifariki.
Mwigizaji huyo wa umri wa miaka 54 alikuwa ameenda kuogelea na mwigizaji mmoja wa kike baada ya kurekodi siku nzima mkasa huo ulipotokea.
Mwigizaji mwenzake Camila Pitanga anasema Montagner alisombwa na mawimbi makali.
Anasema alijaribu kuita wenyeji wafike kumsaidia lakini walichelewa kuchukua hatua kwani mwanzoni walidhani wawili hao walikuwa wanaigiza kisa cha mtu kufa maji mtoni.
Kwenye filamu hiyo, Montagner aliigiza mkulima ambaye mara kwa mara alikabiliana na wavamizi wenye silaha.
Katika moja ya kisa, alipigwa risasi mara kadha na kuonekana kuzama katika mto Sao Francisco, lakini akatokea wiki chache baadaye.
Taarifa zinasema mtu mmoja mmoja hufa maji kila mwaka eneo hilo tangu 2005.

Image copyrightINSTAGRAM/@ANGELICAKSY
Image captionMtangazaji wa runinga Angelica Huck aliandika kwenye Instagram: "Siamini - alikuwa mwigizaji mzuri na mtu mwema pia."

Saa nne baada ya kisa hicho, maafisa wa uokoaji waliupata mwili wa Montagner ndani ya maji, mita 300 (984ft) kutoka eneo ambalo alizama.
Montagner alizaliwa Sao Paulo na alifanya kazi kama mwanasarakasi kabla ya kuwa mwigizaji wa televisheni mwaka 2008.
Hii ilikuwa mara yake ya 12 kuigiza kama mwigizaji mkuu filamu ya runingani.
Filamu yake ya kwanza ya televisheni ambayo alishiriki ilikuwa mwaka 2011, na aliigiza kwenye filamu za kawaida 2012.

Montagner alikuwa amemuoa mwigizaji Luciana Lima kwa miaka 14 na kujaliwa watoto watatu.
Filamu yake ya karibuni zaidi, Um Namorado Para Minha Mulher (Mpenzi wa Kiume wa Mke Wangu), ilizinduliwa wiki mbili zilizopita.