Naibu Waziri Wa Afya, Maendeleo Ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamisi Kigwangalla
SERIKALI imewaagiza watalaam wote wa maabara ambao hawajasajiliwa kufanya hivyo kwa mujibu wa matakwa ya sheria na kuwataka waajiri kutoa ajiri kwa wataalam wasiosajiliwa na baraza la wataalamu wa huduma za maabara za afya.
Hayo yalisemwa leo na Naibu Waziri Wa Afya, Maendeleo Ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamisi Kigwangalla wakati wa uzinduzi wa baraza la wataalamu wa huduma za maabara za afya nchini.

Aidha Dk Kingwangalla amelitaka baraza hilo kuhakikisha linashirikiana na Mamlaka nyingine husika kusimamia ubora wa wataalamu wanaohitimu kwenye vyuo na pia kuwataka wataalam hao kufanya kazi kwa kufuata miiko na maadili waliyoelekezwa katika miongozo mbalimbali ya maabara.
“Wataalamu wote ambao bado hawajasajiliwa na Baraza hili, wafanye hivyo mapema sawa na sheria inayosimamia taaluma hii inavyoelekeza, wale ambao walisajiliwa kwa sheria Na. 12 ya mwaka 1997 kujisajili upya kwa sheria Na. 22 ya 2007 kama ilivyoelekezwa ili wapate vyeti vipya,”alisema Dk Kingwangalla.
Wataalamu wote wa Maabara waliosajiliwa, wametakiwa kuhakikisha wanalipia ada za usajili kila mwaka ili kuhakiki utoaji endelevu wa huduma za maabara, na kupata kibali cha kuendelea kutoa huduma za maabara kwa mwaka mwingine.
Taaluma ya Maabara za Afya ni kati ya taaluma nyeti katika tasnia ya tiba na Sekta ya Afya kwa ujumla kwa kuwa ndio inayotoa dira ya tiba sahihi kwa wagonjwa wanaohitaji tiba.
Dk Kingwangalla alisema Serikali imefanya maboresho katika Sekta ya Afya, ambayo yanalenga kuimarisha na kudumisha huduma bora za afya ya msingi kote nchini.
Miongoni mwa masuala muhimu ni kuweka msingi na taratibu za kuhakikisha watoa huduma za afya wanazingatia Sheria, Kanuni, Miiko na Maadili ili waweze kutoa huduma kwa ufanisi na ubora wa hali ya juu na hatimaye kuwa na Taifa lenye afya bora.