Rais mstaafu wa Tanzania Jakaya Kikwete amelalamika kutokana na kile alichosema ni kutumiwa vibaya kwa picha zake mtandaoni na 'kulishwa maneno'.
Takriban mwaka mmoja tangu astaafu, Bw Kikwete, rais wa awamu ya nne, amesema anafaa kuruhusiwa apumzike.
Aidha, amesema anamuunga mkono Rais wa sasa Dkt John Pombe Magufuli, pamoja na serikali yake.
"Nimestaafu naomba niachwe nipumzike. Nisingependwa kuhusishwa na siasa za mtandaoni dhidi ya Serikali. Namuunga mkono Rais na Serikali yake," ameandika kwenye Twitter.
"Nasikitishwa sana na matumizi mabaya ya picha zangu mtandaoni hususan watu kunilisha maneno kwa kutaka kutimiza malengo yao ya kisiasa."
Bw Kikwete aliondoka madarakani mwishoni mwa mwaka jana baada ya kuongoza taifa hilo kwa miaka kumi.
Tangu aondoke madarakani, ameonekana kujiepusha na masuala ya kisiasa.
Ni nadra sana kwa rais mstaafu Jakaya Kikwete kujibu shutuma ambazo zinahusanishwa naye.
Hivi karibuni watu wamekuwa wakitumia sehemu ya hotuba anazozitoa kumhusisha na ukosoaji wa serikali utendaji kazi wa serikali ya Rais Magufuli.

Bw Kikwete na mrithi wake Dkt MagufuliImage copyrightAFP
Image captionBw Kikwete na mrithi wake Dkt Magufuli

Siku chache zilizopita Kikwete alikuwa anahutubia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na katika hotuba yake alitamka haya: "Unapokuwa mpya watu wanataka mambo mapya pia, lakini yawe mapya ya maendeleo na siyo (mapya) ya kuharibu kule tulikotoka." Sasa watumiaji wa mitandao ya kijamii wamekuwa wakiitumia nukuu hii kuashiria Bw Kikwete alikuwa akiukosoa utawala wa Rais Magufuli