Mke wa Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari, ameonya kuwa huenda asimuunge mkono mumewe kwenye uchaguzi mkuu ujao iwapo kiongozi huyo hatafanya mabadiliko kwenye serikali yake.
Kwenye mahojiano na BBC, Aisha Buhari amesema rais huyo "hawafahamu" wengi wa maafisa wakuu aliowateua serikalini.
Amedokeza kwamba serikali imetekwa, na kwamba kuna "watu wachache" ambao huamua ni nani watateuliwa au kupewa kazi na rais.
Bw Buhari alichaguliwa mwaka jana baada yake kuahidi kukabiliana na ufisadi uliokuwa umekithiri serikali pamoja na ubaguzi na mapendeleo.
Uamuzi wa mke wa kiongozi huyo kusema hayo hadharani umeshangaza wengi, lakini ni ishara ya kiwango cha kutoridhishwa kwa watu na uongozi wa Rais Buhari, anasema mwandishi wa BBC aliyepo Abuja, Naziru Mikailu.
Rais Buhari alitangaza wakati wa kuapishwa kwake kwamba yeye "hamilikiwi na mtu yeyote na anamilikiwa na watu wote".
Kwenye mahojiano na Naziru Mikailu, Bi Buhari alisema: "Rais hawafahamu 45 kati ya 50, kwa mfano, kati ya watu aliowateua na mimi mwenyewe siwafahamu, licha ya kwamba nimekuwa mke wake kwa miaka 27."
Amesema watu ambao hana maono sawa na ya chama tawala cha All Progressives Congress (APC) sasa wanateuliwa kwenye nyadhifa kuu kwa sababu ya ushawishi wa "watu wachache".
"Watu wengine wanaketi manyumbani mwao wakiwa wametulia kisha wanaitwa na kupewa kazi ya kuongoza idara au kuwa mawaziri."

Ayisha Buhari
Image captionBi Ayisha Buhari amesema hatamfanyia kampeni mumewe 2019 mambo yasipobadilika

Aliopulizwa awataje watu waliokuwa wameteka serikali, alikataa na kusema: "Utawajua ukitazama televisheni".
Kuhusu iwapo Rais bado anadhibiti serikali, alisema: "Hilo ni watu wataamua."
Bi Buhari alisema mumewe bado hajamwambia iwapo atawania urais uchaguzi wa mwaka 2019.
"Bado hajaniambia lakini nimeamua, kama mkewe, kwamba mambo yakiendelea hivi hadi 2019, sitatoka kwenda kumsaidia kwenye kampeni na kuomba wanawake wampigie kura kama nilivyofanya awali. Sitafanya hilo tena."
Alipoulizwa ni jambo gani anachukulia kuwa ufanisi mkubwa wa serikali, alisema ni kuimarisha usalama kaskazini mashariki mwa nchi hiyo ambapo serikali imekuwa ikikabiliana na wapiganaji wa Kiislamu wa Boko Haram ambao walianza maasi 2009.
"Hakuna anayelalamika kuhusu kushambuliwa nyumbani kwake. Twashukuru kwamba sasa watu wanaweza kutembea bila kusumbuliwa, na kwenda maeneo ya ibada na kadhalika. Hata watoto Maiduguri wamerejea shuleni," Bi Buhari alisema, akirejerea mji huo ambao wakati mmoja ulikuwa makao makuu ya Boko Haram.