Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene
WANAFUNZI 526,653 sawa na asilimia 94.8 ya waliofaulu mtihani wa darasa la saba mwaka huu, wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani katika shule za sekondari za serikali katika awamu ya kwanza huku 28,638 wakishindwa kupangiwa shule katika awamu ya kwanza.
Kati ya wanafunzi hao, wasichana ni 268,052 sawa na asilimia 94.5 ya wasichana waliofaulu na wavulana ni 258,601 sawa na asilimia 95.2 ya wavulana waliofaulu. Wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani wa darasa la saba mwaka 2016 walikuwa 795,739, huku 244 wakifutiwa matokeo ya mtihani kutokana na udanganyifu.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana mjini hapa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene alisema wanafunzi waliochaguliwa wamegawanyika katika makundi manne likiwemo la shule za bweni kwa wenye ufaulu mzuri ambao waliochaguliwa ni 900 wavulana 480 na wasichana 420.
Alisema kwa shule za bweni za ufundi waliochaguliwa ni 1,005, shule za bweni kawaida ni 780, shule za bweni kwa wenye ulemavu ni 723 na shule za kutwa wanafunzi waliochaguliwa ni 523,245. Alisema jumla ya wanafunzi 3,408 sawa na asilimia 0.6 wamechaguliwa kwenda sekondari za bweni.
Jumla ya watahiniwa 555,291 walifaulu sawa na asilimia 70.36 ya wanafunzi waliofanya mtihani, kati yao wasichana ni 238,753 sawa na asilimia 51.1 na wavulana 271,538 sawa na asilimia 48.9.
Ufaulu umeongezeka kwa asilimia 2.52 ukilinganisha na asilimia 67.84 kwa mwaka 2015. Simbachawene alisema katika uchaguzi huo, wanafunzi 28,638 hawakuchaguliwa katika awamu ya kwanza, na kuitaja mikoa ambayo wanafunzi wamebaki ni Dar es Salaam (18,820), Arusha (4,752), Songwe (1,465), Kigoma (1,208), Manyara (1,141), Lindi (608), Mbeya (406) na Katavi (238).
Aidha, waziri huyo alisema kati ya wanafunzi 1,060,588 walioanza darasa la kwanza 2010, wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani wa darasa la saba mwaka 2016 ni 795,739 sawa na asilimia 75 ya wanafunzi walioandikishwa wakiwemo wasichana 422,562 sawa na asilimia 53.1 na wavulana 373,177 sawa na asilimia 46.9 ya waliosajiliwa.
Akizungumzia udanganyifu, alisema watawavua madaraka kwa waliokuwa waratibu elimu kata na walimu wakuu, kuwashitaki mahakamani na kupeleka mashauri yao Tume ya Utumishi ya Walimu, baada ya udanganyifu kuongezeka ambako watahiniwa 244 wamefutiwa matokeo mwaka 2016 ikilinganishwa na wanane wa mwaka jana.
Alizitaja shule zilizohusika kwenye udanganyifu huo ni Shule ya Tumaini na Little Flower za Sengerema mkoani Mwanza, Mikahamakumi iliyopo Sikonge, Tabora ambazo ni za binafsi, wakati za serikali ni Kondi Kasandalala iliyopo Sikonge, Tabora, Qash iliyopo Babati na St Getrude iliyopo Madaba mkoani Ruvuma.
Aidha, alisema 10 bora za serikali ni Kazunzu iliyopo Halmashauri ya Buchosa (Mwanza), Mwanahegele ya Maswa (Simiyu), Huruma ya Mbinga (Ruvuma), Kabanga ya Ngara (Kagera), Butumba B (Jiji Mwanza), Masoko ya Kilwa (Lindi), Lyambamgongo ya Bukombe (Geita), Kilimani ya Geita Vijijini, Magufuli ya Chato na Nkome ya Geita Vijijini, Geita.
Alisema shule 10 zilizofanya vibaya ni Chohelo ya Mvomero (Morogoro), ambayo ni ya mwisho kitaifa ikifuatiwa na shule za Iloliento, Longido (Arusha), Mwalebi na Nchilila Meatu (Simiyu), Magingi ya Mvomero, Kilole ya Lushoto, Tanga, Zege ya Korogwe, Tanga na shule tatu za Lubchi, Kitengo na Mgata za Morogoro vijijini.