KAMPALA, UGANDA: Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda, wameanza kuondoka kutoka chuoni hapo baada ya Rais Yoweri Museveni kutangaza kifungwe mara moja jana Jumanne jioni.
Rais Mseveni alisema amechukua hatua hiyo “kuhakikisha usalama wa watu na mali.”
Chuo kikuu hicho kilikuwa kimekumbwa na vurugu kutokana na mgomo wa wahadhiri na wanafunzi.

Chama cha wahadhiri Jumatatu kiliamua kuendelea na mgomo hadi wahadhiri walipwe marupurupu ya miezi minane ambayo yamefikia Sh32bn (dola 9.2 milioni za Marekani).
Wanafunzi walianza kugoma tangu jana Jumanne, na walitaka kukutana na Rais Museveni badala ya Mwenyekiti wa Baraza Simamizi ya Chuo chini ya Uenyekiti wa Dkt Charles Wana-Etym.
Naibu chansela wa chuo hicho Prof Ddumba Ssentamu wiki iliyopita alikuwa amewasihi wahadhiri wakubali kurejea kazini huku suluhu ya kudumu ikiendelea kutafutwa.